UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116539

E-mail: press@ikulu.go.tz

Website:  www.mawasilianoikulu.go.tz  

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Heshimuni ahadi zetu kwa masikini, Rais Kikwete aziambia nchi tajiri

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, amezitaka nchi zilizoendelea na tajiri duniani kuheshimu ahadi ya nchi hizo ya kuchangia kiasi cha dola bilioni 40 katika jitihada za kupunguza vifo vya akinamama na watoto duniani kwa kuhakikisha zinatoa fedha hizo na kwa wakati ili kupunguza vifo vya mamilioni ya akinamama na watoto.

Aidha, Rais Kikwete amezitaka nchi masikini na zinazoendelea duniani kuhakikisha kuwa endapo fedha hizo zinapatikana na kutolewa basi zitumiwe vizuri na nchi zinazopewa fedha hizo kwa ajili ya shughuli iliyokusudiwa ya kuokoa maisha ya watoto na akinamama hasa katika nchi masikini na zinazoendelea.

Rais Kikwete ametoa miito hiyo jana, Jumatano, Januari 26, 2011, wakati anafungua na kuendesha Mkutano wa Kwanza wa Tume ya Umoja wa Mataifa Kuhusu Afya ya Akinamama na Watoto ambayo anaiongoza kwa ushirikiano na Waziri Mkuu wa Canada, Mheshimiwa Stephen Harper.

Katika ujumbe wake mzito zaidi katika hotuba yake ya ufunguzi ambao ameurudia katika majadiliano, katika ufungaji wa mkutano na katika mkutano na waandishi wa habari ambavyo vyote vimefanyika mjini Geneva, Uswisi, Rais Kikwete amewaambia makamishna na waalikwa katika mkutano huo:

Tunazitaka nchi zilizoendelea kuheshimu ahadi yake ya kutoa zaidi ya dola bilioni 40 ili kugharimia mpango kakati wa kuboresha afya ya akinamama na watoto duniani katika miaka mitano iyajo.”

Rais Kikwete ameongeza: “Ni matumaini yangu vile vile kuwa utakuwepo uwajibikaji mkubwa zaidi kwa wadau wote watakaopokea fedha hizo zikiwamo Serikali, taasisi za kimataifa, mashirika yasiyokuwa ya kimataifa (NGO’s) katika matumizi ya fedha hizo na raslimali nyingine ambazo watapata katika kupambana na vifo hivyo,”

Tume inayoongozwa na Rais Kikwete na Waziri Mkuu Harper inalenga kuongeza kasi ya kuokoa maisha ya akinamama na watoto duniani kwa kuhakikisha Malengo ya Maendeleo ya Milenia Duniani hasa yake malengo yanayohusika na afya yanafikiwa kama ilivyopangwa, yaani mwaka 2015.

Kikao cha jana pia kilihutubiwa na Mheshimiwa Harper mwenyewe na makamu wenyeviti wenza ambao ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dkt. Margaret Chan na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano ya Simu Duniani, Dkt. Hamadoun Toure. Tume hiyo itatoa ripoti yake ya mwisho mwezi Mei mwaka huu.

Mwisho.

Imetolewa na:

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais,

Safarini, GENEVA.

27 Januari, 2011