THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

OFFICE OF THE PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

    Fax. No. 255-22 2113425                                                                                                              The State House,                                                                   

    Tel: 255-22-2116539/2116913                                                                                                       P.O. Box 9120,                                                                                                                                                                                   

                                                                                                                                                            DAR ES SALAAM.

  E-mail:  press@ikulu.go.tz          

 

 

                                  

 

Premi Kibanga,

Copenhagen, Denmark

2 March, 07

 

Mabadiliko ya kisiasa na kiuchumi nchini Tanzania ni kipimo bora na mfano  wa kuigwa na nchi zote barani Afrika.

 

Waziri Mkuu wa Denmark Bwana. Anders Fogh Rasmusssen amemweleza Rais Jakaya Mrisho Kikwete jana (1.March .07) wakati wa mazungumzo mjini hapa.

 

“Umefanya mabadiliko makubwa na tumevutiwa sana na matokeo yaliyopatikana hadi sasa, tunatiwa moyo sana na serikali yako, imeweka kiwango cha mafaniko ambacho kinafaa kuigwa na nchi zote barani Afrika”. Amesema na kuongeza kuwa “ Kutokana na jitihada hizo za Tanzania, tumeamua kutayarisha sera mpya ya Afrika yenye lengo la kukuza mahusiano yetu kwa miaka ijayo”.

 

Bwana Rasmussen amesema Denmark imeazimia kuongeza misaada kwa nchi za Kiafrika ili kujenga mahusiano imara yenye lengo la kuendeleza mabadiliko haya ya kisiasa na kiuchumi,  ili kujenga mazingira bora  katika masoko, biashara  na pia katika kukuza amani na utulivu barani Afrika.

 

Rais Kikwete amemweleza kwa undani jitihada za serikali yake katika kuendeleza na kuimarisha marekebisho ya kisiasa ambapo ameelezea hatua zilizofikiwa katika maswala ya utawala bora haswa suala la kupambana na rushwa,  swala ambalo Denmark imesema imeridhishwa sana nalo na kwamba ni swala lililowazi kuwa  serikali ya Tanzania  imedhamiria na hivyo kuifanya Denmark nayo kurejea ahadi zake za kuendelea kuisaidia Tanzania bila mjadala zaidi.

 

“Mahitaji yote yakikamilika na kuwa wazi Denmark itatoa msaada wake kama ilivyokwisha kubalika” Amesema Bw. Rasmussen na kuongeza kuwa mbali na kuongeza misaada kwa Tanzania, Denmark itatoa kipaumbele kwa elimu kwa watoto wa kike ili kuimarisha nafasi za wanawake katika maendeleo.

 

Mwishoni mwa mwaka jana Denmark ilizuia mchango wake wa asilimia ishirini kwa Tanzania kwa kile kilichodaiwa kuchelewa kuwakilisha bungeni mswaada wa marekebisho ya sheria ya kupambaba na rushwa Tanzania, muswaada ambao tayari umeshawakilishwa mwezi Februari mwaka huu na unatarajiwa kuwa ufikapo mwezi wa Mei utakuwa umekamilika.

 

 

“Tutaendeleza marekebisho haya na pia  tumedhamiria kujenga uchumi imara na tulivu lakini tuna changamoto kubwa ya kuikomboa sekta binafsi na kuijengea mazingira mazuri kama vile kupata mikopo na mitaji.”

 

Amesema Tanzania imeingia katika awamu ya pili ya marekebisho ya sekta ya fedha yenye lengo la kuwezesha wananchi na sekta binafsi kupata mitaji na mikopo kwa lengo la kuendeleza sekta za kilimo, utalii, madini,  nishati na sekta mbalimbali za kutoa huduma.

 

Viongozi pia wamezungumzia maswala mbalimbali ya Afrika ikiwemo swala la Dafur, Zimbabwe na juhudi mbalimbali za Tanzania katika kuleta amani na utulivu barani.

 

Tanzania imekuwa mstari wa mbele barani katika kuleta amani na utulivu, mambo ambayo ni muhimi kwa maendeleo. Tunaunga mkono na tutazidi kusaidia Afrika katika swala hili” Amesema.

 

Rais anatarajia kukamilisha ziara yake hapa Denmark leo kwa kukutana na mume wa Malkia Margrette II wa Denmark, Prince Henrik na viongozi wengine wa juu serikalini akiwemo Waziri wa Ushirikiano wa Maendeleo Mama Ulla Tornaes.Rais anatarajiwa kurejea nyumbani kesho (3.02. 07)

Ends