DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail:  ikulumawasiliano@yahoo.com

              press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

JK: Kweli uchumi unakua,

lakini sisi bado masikini

 

 

Na Mwandishi Maalum,

 

PAMOJA na kupokea pongezi za China kuhusu kukua vizuri na haraka kwa uchumi wa Tanzania, Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa bado Tanzania ni nchi masikini mno na maisha ya wananchi bado ni magumu.

 

Amesema kuwa kupanda mno kwa bei za mafuta katika miaka ya karibuni pia kumechangia kuzidisha ugumu wa maisha kwa wananchi.

 

“Ni kweli Tanzania ni nchi ya amani na isiyoyumba. Uchumi wetu umekuwa unakua kwa wastani wa asilimia saba kwa miaka kadhaa sasa. Lakini bado maisha ya wananchi wetu ni magumu. Bado yetu ni nchi masikini,” Rais Kikwete ameuambia ujumbe wa Chama cha Kikomunisti cha China leo (Alhamisi, Septemba 18, 2008) na kuongeza:

 

Pato la wastani ya wananchi wetu ni dola za Marekani 500 tu, na ongezeko la bei la mafuta katika miaka ya karibuni limeyafanya maisha ya wananchi wetu kuwa magumu zaidi.”

 

Rais Kikwete alikuwa anazungumza na ujumbe wa Chama cha Kikomunisti cha China wakati alipokutana nao kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA). Rais Kikwete alikuwa njiani kurejea Dar es Salaam baada ya kumaliza ziara ya Mkoa wa Manyara.

 

Ujumbe huo uliokuwa katika ziara ya siku tatu ya Tanzania kwa mwaliko wa Chama cha Mapinduzi (CCM) umeondoka mara tu baada ya mazungumzo hayo kwenda Uganda kuendelea na ziara yake katika Afrika. Uliwasili nchini kutokea Afrika Kusini juzi (Jumanne, Septemba 16, 2008), na baada ya Uganda unakwenda Gabon na Nigeria.

 

Rais Kikwete ametoa ufafanuzi huo kuhusu tafsiri ya uchumi wa Tanzania baada ya kiongozi wa ujumbe huo, He Yong, ambaye ni Katibu wa Sekretariati ya Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti kuimwagia sifa nyingi Tanzania, uchumi wake na uongozi wa Rais Kikwete.

 

Amesema He Yong: “Yenu ni jamii iliyotulia, isiyoyumba. Tanzania ni moja ya nchi zenye chumi zinazokua haraka kwenye Bara hili. Yote hayo yametokana na uongozi wako imara ambao umeongeza uwezo wa utawala bora wa nchi yenu.”

 

Ameongeza: “Ni jambo la kutia moyo na kufurahisha kwamba kwa miaka 10 sasa, uchumi wenu umekuwa unakua haraka na kwenda mbele. Tunapenda kuelezea husuda yetu kwa uongozi wako ambao umepelekea mafanikio haya yote.”

 

He Yong amesema kuwa ziara hiyo inalenga kuongeza nguvu nyingine katika kuimarisha uhusiano wa miaka 44 kati ya Tanzania, na kuwa ujumbe wake umepokewa vizuri na kufanya mazungumzo yenye tija na wenyeji wao, yaani Chama cha Mapinduzi.

 

 

 

Mbali na kufanya mazungumzo na CCM, ujumbe huo pia umetembelea mji wa Bagamoyo, kijiji cha Mwenge cha Dar es Salaam na Makao Makuu ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), iliyojengwa kwa mkopo kutoka China.

 

Kwa upande wa Tanzania, mazungumzo hayo ya leo yamehudhuriwa pia na Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa pamoja na Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko, Mary Nagu.

 

Rais Kikwete pia ametumia nafasi ya mazungumzo hayo kumweleza kwa undani hali ya kiuchumi nchini, na hasa hatua zipi Tanzania inastahili kuzichukua kuongeza kasi ya kukua kwa sekta ya kilimo, ambayo alisema ndiyo itakuwa mkombozi wa kweli kweli wa Mtanzania.

 

Rais pia amemwelezea He Yong kuhusu hali ya TAZARA akisema kuwa reli hiyo imekuwa inakabiliwa na matatizo mengi kwa sababu ya menejimenti isiyoridhisha.

 

Kwa kweli tumeiendesha vibaya TAZARA. Kabla ya kifo cha Rais wa Zambia tulikuwa tumepanga kukutana kuzungumzia hili. Lakini sasa nitakutana na Makamu wa Rais kutafuta namna ya kuimarisha uongozi wa TAZARA,” amesema Rais na kuongeza:

 

Karibuni, kama umesikia tumekodisha Reli ya Kati hapa kwetu. Ni mawazo yangu kuwa tufanye hivyo hivyo na TAZARA. Ni mawazo yangu vile vile kupata kampuni ya China kusaidia kuiendesha reli hiyo. Wakati huo ukifika bila shaka mtatusaidia kutafuta kampuni ya namna hiyo.”

 

 

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

18 Septemba, 2008