DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mhe. Rais Jakaya Kikwete amemteua Jaji Frederick Mwita Werema kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 

Aidha, Mhe. Rais Kikwete amemteua Bwana George Mcheche Masaju kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 

Uteuzi huo unaanza leo, Jumanne, Oktoba 20, 2009.

 

Kabla ya uteuzi wake, Jaji Werema alikuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Biashara.

 

Jaji Werema anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Bwana Johnson Mwanyika ambaye yuko kwenye likizo ya kustaafu kwa mujibu wa sheria.  Bwana Mwanyika aliteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Desemba, mwaka 2005.

 

Naye Bwana Masaju kabla ya uteuzi wake alikuwa Mshauri wa Sheria wa Rais, Ikulu.

 

Wakati huo huo, Mhe. Rais Kikwete kesho, Jumatano, Oktoba 21, 2009 atawaapisha maofisa hao wawili waandamizi wa Serikali pamoja na Makatibu Wakuu wa Wizara za Serikali ambao aliwateua jana, Jumatatu, Oktoba 19, 2009.

 

Maofisa hao watakaoapishwa ni Jaji Frederick M. Werema kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali; Bwana David Kitundu Jairo kuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati na Madini; Bwana Sazi Salula kuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa; na Bwana Mbarak M. Abdulwakil kuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

 

Wengine watakaoapishwa ni Bwana Christopher Sayi kuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Maji na Umwagiliaji; Bwana Sethi Kamuhanda kuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo; Bwana Prosper Mbena kuwa Katibu wa Rais, na Bwana George Masaju kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 

Shughuli ya kuapishwa itaanza saa sita mchana, Ikulu, Dar es Salaam.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

20 Oktoba, 2009