DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatatu, Oktoba 5, 2009, ametoa mwito maalum kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi kujiandikisha, ili waweze kushiriki kuwapigia kura viongozi wa serikali za mitaa.

 

Mhe. Rais Kikwete ametoa mwito huo wakati yeye mwenyewe alipojiandikisha katika Kituo cha Shule ya Msingi ya Bunge karibu na Ikulu, Dar e Salaam, ili aweze kupiga kura katika uchaguzi huo uliopangwa kufanyika nchini kote baadaye mwezi huu, Oktoba 25, 2009.

 

Aidha, Mhe. Rais ametaka wananchi kuwakemea baadhi ya watu wachache ambao wamekuwa wanafanya fujo katika zoezi la uteuzi wa wagombea katika uchaguzi huo na kwenye zoezi la uandikishaji.

 

            mesema Mhe. Rais baada ya kuwa amejiandikisha: “Niwaombeni Watanzania kote nchini kujitokeza kwa wingi kujiandikisha. Hatari ni kwamba watu wanaweza kupuuza uchaguzi huo wakingojea ule wa Rais na wabunge mwakani.”

 

Amesisistiza: “Lakini kila uchaguzi una uzito wake na viongozi hawa tutakaowachagua baadaye mwezi huu ndiyo viongozi muhimu katika maisha yetu. Hawa ndio tunaishi nao kila siku.  Kama kuna shida ya mtaro wa maji machafu, ama shinda ya ukosefu wa umeme, ama hakuna maji, hawa ndio watu wa kutushughulikia.”

 

 

“Hivyo, nawaombeni Watanzania tujitokeze kwa wingi kujiandikisha na siku ile ya Oktoba 25, tujitokeze kwa wingi kupiga kura. Watu wasije kupuuza zoezi hilo la sasa kwa sababu ya kungojea uchaguzi wa mwakani. Ni zoezi muhimu sana kwa sababu hili ndilo linatupa wenyekiti wetu wa mitaa na wenyekiti wetu wa vijiji,” amesema Mhe. Rais na kusisistiza:

 

“Hawa ndio viongozi wa shida zetu za mchana na usiku. Nawaombeni sana, na hasa wakazi wa mijini, kujitokeza kujiandikisha. Nawaombeni pia vyombo vya habari kusaidia katika kuhamasisha uandikishaji na upigaji kura.”

 

Mhe. Rais amesisitiza kuwa katika kuboresha mfumo wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, zamu hii Serikali imeanzisha daftari la wapigaji kura badala ya huko nyuma ambako watu walikuwa wanapiga kura bila kujiandikisha kwenye daftari.

 

“Uchaguzi uliopita hakukuwapo na daftari la wapigaji kura. Lakini ili kuondoa malalamiko ya aina yoyote, zamu hii tumeanzisha daftari hilo.”

 

Alipoulizwa na mwandishi wa habari juu ya fujo ambazo zimekuwa zinaripotiwa na vyombo vya habari kuhusiana na uchaguzi huo, Mhe. Rais amesema:

 

“Binafsi nawashangaa watu wanaofanya fujo.  Shughuli yenyewe haitakiwi kuwa na fujo. Ni jambo lisilokuwa na maana na kwa kweli ni ukosefu wa busara watu kufanya fujo katika zoezi hili. Tukemee jambo hili. Tuwakemee watu hawa wanaofanya fujo za kijinga. Ni lazima waache uhuni.”

 

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

05 Oktoba, 2009