DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo, Jumatatu, Machi 29, 2010, amepokea vifaa mbalimbali vya msaada kutoka kwa Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China katika Tanzania, Mheshimiwa Liu Xinsheng.

 

Vifaa hivyo vyenye thamani ya shilingi milioni 51 vimekabidhiwa kwa Mheshimiwa Rais katika hafla fupi iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, na ni kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.

 

Vifaa hivyo ni pamoja na baiskeli, pikipiki, redio, mipira, mabati, vyerehani, jozi za kandambili, vyombo vya muziki, mashine za maji, televisheni, na jozi za sapatu.

 

Akikabidhi vifaa hivyo, Balozi Xinsheng amesema kuwa vifaa hivyo vimetolewa kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo ya Tanzania, ambayo uchumi wake uliweza kukua kwa kasi ya asilimia 5.8 mwaka jana, pamoja na kwamba Tanzania, kama nchi nyingine duniani, ilikabiliwa na zahama ya uchumi.

 

Mheshimiwa Rais amemshukuru Balozi huyo kwa misaada mbalimbali ambayo nchi ya China imekuwa inatoa kwa Tanzania tokea mwaka 1964 wakati nchi hizo mbili zilipoanzisha uhusiano wa kibalozi.

 

“Mmetusaidia kwa mambo mengi yahusuyo shughuli za maendeleo ya kiuchumi, kijamii, na kiulinzi wa nchi yetu. Tunakushukuru sana kwa misaada yenu viwanda, Reli ya Tazara, kilimo, afya na hata kuimarisha ulinzi wa taifa letu. Leo umetoa misaada hii ya kunufaisha wanafunzi na jamii kwa jumla. Nimeamua tupeleke misaada hiyo Wilayani Kilosa kusaidia juhudi za kukabili athari za mafuriko na kusaidia shughuli za maendeleo kwa jumla Wilayani kote.

 

Mheshimiwa Rais ameelekeza Ofisi ya Rais, Ikulu ishirikiane na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro na Mkuu wa Wilaya ya Kilosa kupanga utaratibu wa kugawa vifaa hivyo.

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

29 Machi, 2010