UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama nchini, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Ijumaa, Julai 30, 2010, amekutana na kuzungumza na wazee wakongwe wa vita nchini na wanachama wa Tanzania Legion and Club.

 

Aidha, Rais Kikwete ambaye ni Mlezi wa Tanzania Legion and Club amekula chakula cha mchana na wazee hao katika shughuli iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam.

 

Katika mazungumzo hayo, wazee ambao ni wawakilishi wa wenzao kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania wamemweleza Mheshimiwa Rais kuhusu changamoto mbali mbali zinazokikabili chama hicho.

 

Moja ya changamoto ambazo wamemweleza Mheshimiwa Rais ni pamoja na wanachama hao kutokulipwa mafao yao ya vita kutoka taasisi ya Royal Commonwealth Ex-Services League ya Uingereza. Wazee hao walipigana upande wa majeshi ya Uingereza katika Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.

 

Wanachama hao pia wamemweleza Mheshimiwa Rais Kikwete jinsi wanachama hao wanavyosumbuliwa katika kupata usajili wa Bodi yao ya uongozi ambao wanasema kuwa ni Bodi iliyochaguliwa kihalali katika mkutano halali wa chama chao.

 

Aidha, wazee hao wamemweleza Rais Kikwete matatizo yanayoikabili klabu hiyo na wanachama wake katika jitihada zao za kuendeleza miradi mbalimbali na pia wameomba msaada wa Serikali katika kuwawezesha ili wafanikishe mkutano wao mkuu ambao umekuwa ukiahirishwa kutokana na ukosefu wa fedha.

 

Wazee hao ambao wana umri wa kati ya miaka sabini na miaka 112, pia wamemshukuru Rais Kikwete kwa kupata muda wa kuwaalika na kuzungumza nao katika kitendo ambacho wamekieleza kuwa ni cha kwanza kufanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika historia ya Tanzania Legion and Club.

 

Akizungumza na wazee hao, Rais Kikwete amewapa ushauri wake kwa namna ya jinsi ya kukabiliana na changamoto zinazoukabili umoja wao na wanachama wake.

 

Kuhusu suala la mafao yao, Rais Kikwete ameielekeza Wizara ya Ulinzi na Kujenga Taifa kuchukua hatua za kutafuta majawabu ya tatizo hilo kwa kutumia Ubalozi wa Tanzania katika Uingereza.

 

Kuhusu mwelekeo ya baadaye wa chama hicho, Rais Kikwete amewashauri wanachama hao kujenga mazingira ya kisheria na kitaasisi ya kukiwezesha chama hicho kuendelea kuwapo kwa miaka mingi ijayo kwa sababu mfumo na muundo wa sasa ni wa hiari zaidi kuliko kisheria.

 

Naamini katiba ya sasa ya Tanzania Legion haikipi chama hiki uhai wa kudumu hata kama sote tutakuwa hatupo tena duniani. Ni lazima tupate ushauri wa wanasheria wa jinsi ya kukipa chama hiki uhai wa kudumu,“ Mheshimiwa Rais amewaambia wazee hao na kuongeza:

 

Moja ya njia za kufanya hivyo ni kuibadilisha Legion kuwa kampuni ambako watu wanaweza kununua hisa wakiwamo watoto wetu, wajukuu zetu na hata wanajeshi wengine wa Tanzania.”

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

30 Julai, 2010