DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

RAIS Barack Obama wa Marekani amempongeza Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa kufanikisha mchakato wa maridhiano ya Zanzibar na hasa kwa mafanikio makubwa ya kura ya maoni ya kuundwa kwa Serikali ya Umoja Tanzania Visiwani.

 

Rais Obama ametoa pongezi hizo kwa Rais Kikwete kupitia ujumbe maalum uliowasilishwa kwake leo, Jumanne, Agosti 17, 2010, na Balozi wa Marekani katika Tanzania, Mheshimiwa Alfonso E. Lenhardt katika mazungumzo kati ya viongozi hao Ikulu, Dar es Salaam.

 

Katika salamu hizo, Rais Obama amemwambia Rais Kikwete: “Kwa niaba ya wananchi wa Marekani, natoa salamu zangu za pongezi kwako wewe (Rais Kikwete), kwa viongozi wa Zanzibar, kwa wananchi wa Zanzibar, na kwa Watanzania wote kwa kufanikisha kura ya maoni ya Serikali ya Umoja ya Julai 31, 2010.”

 

Nakumbuka majadiliano yetu kuhusu azma yako ya kuendeleza maridhiano na utawala wa sheria katika Zanzibar wakati tulipokutana katika Ikulu ya Marekani Mei mwaka jana, 2009,” Rais Obama amemwambia Rais Kikwete na kuongeza:

 

“Ni jambo la kutia moyo kwamba katika kipindi kifupi tu cha zaidi kidogo tu ya mwaka mmoja, uongozi wako, azma ya pamoja ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, wanachama wa taasisi zisizokuwa za Kiserikali, jumuia ya dini, na vyama vya siasa imefanikisha kupiga hatua kubwa sana katika kuleta amani ya kudumu iliyojidhihirisha katika kura ya maoni ya asilimia theluthi mbili kuridhia kuundwa kwa Serikali ya Umoja.”

 

Wakati walipokutana katika Ikulu ya Marekani Mei 21, mwaka jana, 2009, Rais Kikwete alimwahidi Rais Obama kuwa uongozi wa Tanzania ungefanya kila linalowezekana kumaliza mvutano wa kisiasa katika Visiwa vya Unguja na Pemba kwa njia za amani na maelewano.

 

Ameongeza Rais Obama katika pongezi hizo kwa Rais Kikwete: “Bado ipo kazi kubwa ya kufanya kwa kadri Uchaguzi Mkuu wa Oktoba unavyokaribia, lakini nina imani kabisa, kwa uongozi wako endelevu na azma isiyoyumba ya wananchi wa Tanzania katika kuleta amani ya kudumu, hali ya baadaye ya matumaini iko mbele yetu. Natumaini kuwa tutaendelea kushirikiana na kufanya kazi pamoja katika shabaha zetu nyingi na za pamoja.”

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

17 Agosti, 2010