DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Na Mwandishi Maalum, Mwanza

 

RAIS Jakaya Mrisho Kikwete ametaja misingi mikuu mitatu iliyowekwa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere katika kulijenga taifa la Tanzania, misingi ambayo Rais amesema ndiyo kumbukumbu kuu ya Watanzania kwa Mwalimu.

 

Aidha, Rais Kikwete amewashangaa Watanzania ambao wanabeza uhuru wa Tanzania na kufurahia wakati jina la Tanzania linaposhambuliwa na wageni.

 

Ameitaja misingi hiyo mikuu kuwa ni uhuru, umoja wa taifa la Tanzania, na safari ya kujenga maisha bora kwa kila Mtanzania iliyoanza hata kabla ya Tanganyika kupata uhuru wake rasmi Desemba 9, 1961.

 

Rais Kikwete ameyasema hayo mjini Mwanza jioni ya jana, Jumamosi, Oktoba 3, 2009 alipozungumza na vijana wa CCM ambao wanaondoka mjini Mwanza leo kwenda Butiama, Mkoani Mara, kwa Matembezi Maalum ya kumuezi Mwalimu kwenye kumbukumbu ya miaka 10 tokea kufariki kwake, Oktoba 14, 1999.

 

Vijana 166 kutoka mikoa yote ya Tanzania wanashiriki katika Matembezi hayo ya siku 10 na yatakayopitia njia ile ile ambayo Mwalimu Nyerere alitembea mwaka 1967 katika kuunga mkono na kuhamasisha Azimio la Arusha.

 

Kauli mbiu ya Matembezi hayo ni “Uhuru na Kazi” na miongoni mwa mambo ambayo vijana hao watafanya njiani ni kukarabati Shule ya Msingi ya Mwisenge ambako Mwalimu Nyerere alipata elimu yake ya msingi.

 

Rais Kikwete amesema kuwa urithi mkuu ambao Mwalimu aliwaachia Watanzania ni misingi hiyo mikuu ambayo imeendelea kulifanya Taifa la Tanzania kuwapo na kuwa imara.

 

Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa kila taifa duniani linalo waasisi wake ambao wanastahili kuendelea kukumbukwa siyo tu kwa uasisi pekee, lakini kwa mambo ambayo waliyasimamia, waliyaamini na waliyajenga.

 

“Wamarekani wale wanaye George Washington… sisi tunaye Mwalimu Julius Kambarage Nyerere… na kila nchi ina mwasisi wake ambaye anakumbukwa kwa aliyoyasimamiaamesema Mwalimu na kuongeza:

 

“La kwanza la kumkumbuka Mwalimu ni uhuru wa nchi yetu.  Huyu alikuwa ni kiongozi aliyeambiwa achague kati ya siasa ama kazi ya ualimu… huyu mzee wetu akachagua siasa na utumishi wa umma bila hata kujua atakula nini

 

“Akachagua kupigania uhuru wa nchi yetu. Kama mnavyojua nyote hii kazi ya siasa ni kamari..unakwenda kugombea ukijua kuna kupata ama kukosa..lakini yeye alifanya uamuzi sahihi wa kupigania uhuru

 

Rais Kikwete amesema kuwa uhuru siyo mipaka bali ni heshima ya nchi na ndiyo maana Tanzania haitasita kumkabili yoyote ambaye atajaribu kuchezea uhuru huo.

 

Amesisitiza: “Mwaka 1978, yule msanii na profesa wa historia na jiografia, Idi Amin alivamia nchi yetu…. na sisi tukamfurumusha ili kulinda uhuru wetu na wako wenzetu ambao walipoteza maisha yao kwa ajili ya kulinda uhuru wetu. Wamelala Kaboya (Mkoa wa Kagera) na tutaendelea kuwaenzi kwa sababu walijitolea kulinda uhuru wetu

 

Rais Kikwete pia amewashangaa wale wote ambao wanafurahia wakati heshima ya Tanzania inapobezwa na wageni. “Uhuru siyo mipaka kama nilivyosema. Uhuru ni heshima ya taifa letu. Wako wale wenzetu wanaofurahi wakati wageni wanaposhambulia nchi yetu. Ni wajibu wetu sote kuhakikisha kuwa uhuru wetu hauchezewi na mtu yoyote

 

Kuhusu umoja wa taifa, Rais Kikwete amesema kuwa Mwalimu alihakikisha kuwa uhuru wa nchi unazaa umoja ili nchi iwe moja na isigawanyike vipande vipande kwa sababu yoyote ile.

 

“Aliondoa viashiria vyote vya kuvunja umoja wa taifa tokea mwanzo kabisa. Aliondoa uchifu ili kuondoa nguvu za ukabila. Alitambua hatari ya dini na akataifisha shule zote za dini ili vijana wetu waelimishwe na kulelewa kama vijana wa taifa moja na siyo vijana wa dini tofauti

 

Rais Kikwete amesema kuwa hata kabla ya uhuru, Mwalimu alitambua ili uhuru na umoja viweze kudumishwa ni lazima wananchi wake wapate maisha bora na ndiyo maana akawatambua maadui wakuu watatu – ujinga, maradhi na umasikini- na njia za kukabiliana na maadui hao.

 

“Wapo watu wanaobeza kuwa hii sera ya maisha bora imeletwa na akina Kikwete. Sisi tumeendeleza sera ile ile ambayo taifa hili limekuwa linatekeleza tokea uhuru wetu… na wala kazi hii haitaishia kwangu mimi, hata wale viongozi watakaonifuata wataendeleza sera hii kwa sababu kazi ya kujenga maisha bora kwa wananchi haihishi, haina kikomo

 

Amesisitiza Rais Kikwete: “Tunapojenga shule tunapambana na ujinga, tunapojenga chuo kikuu kipya pale Dodoma tunapambana na ujinga… tunapopanua huduma za afya tunapambana na maradhi, tunapoelekeza nguvu zetu kupambana na ukimwi tunapambana na maradhi…tunapojenga barabara tunapambana na umasikini, tunapoanzisha Kilimo Kwanza tunapambana na umasikini…”