UNITED REPUBLIC OF
TANZANIA
DIRECTORATE OF
PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116539 E-mail: press@ikulu.go.tz Website: www.mawasilianoikulu.go.tz Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S
OFFICE, THE STATE HOUSE, P.O. BOX
9120, DAR ES SALAAM. Tanzania. |
TAARIFA KWA VYOMBO
VYA HABARI
Anzisheni mashamba ya kunenepesha
ng’ombe – Rais Kikwete
Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete
ametaka kutengwa kwa maeneo makubwa
ya kutosha kila mkoa ili
kuanzisha mashamba ya kunenepesha ng’ombe kama moja
ya njia za
haraka za kuwatoa wafugaji katika umasikini, kuandaa mazingira mwafaka ya uwekezaji
katika sekta ya mifugo na
kudhibiti uzururaji na mifugo na
wachungaji.
Aidha, Rais Kikwete ametaka
kuanzishwa kwa
mageuzi ya sekta za mifugo
na uvuvi na kusisitiza kuwa
taifa la Tanzania haliwezi kuendelea na ufugaji
wa asili usiokuwa na tija
na wenye kujenga mazingira ya mfugaji kutumikia
ng’ombe badala ya ng’ombe kumtumikia
mfugaji.
Vile
vile Rais ameelekeza zichukuliwe hatua haraka za
kuwasaidia wachungaji mifugo wa
Tanzania kuweza kubadilika na kuwa wafugaji.
Rais Kikwete ametoa maelekezo hayo leo, Jumatano,
Machi 30, 2011, wakati alipotembelea na kuzungumza na viongozi
wa Wizara ya Mifugo na
Uvuvi na taasisi zake katika
mwendelezo wa ziara zake kutembelea
Wizara mbalimbali za Serikali kufuatilia
utekelezaji wa maamuzi ya Serikali.
“Mashamba ya kunenepesha ng’ombe ndio eneo
ambako mageuzi yetu katika sekta
ya mifugo yanapoanzia.
Na hili ndilo jambo ambalo nitalidai
kwa bidii kutoka kwa Wizara
hii na viongozi
wake,” amesema Rais Kikwete katika kusisitiza umuhimu wa kuanzishwa
kwa mashamba hayo (feed lots ama pasture development) na kuongeza:
“Tafuteni ardhi ya kutosha katika
kila mkoa, kuanzia kiasi cha hekta 100 kwa
ajili ya kuwasaidia wananchi kuanzisha mashamba ya mbegu za
malisho na kunenepesha ng’ombe. Hili litasaidia watu kuacha uzururaji nchi nzima kutafuta
malisho kwa
ajili ya mifugo yao kwa
sababu kimsingi kama watu wanapo
mahali pa kulisha mifugo yao hawatahama
tena. Na isitoshe,
iko siku kutakuwa hakuna mahali ya kuhamia
kila kukicha.”
Amesema kuwa mashamba hayo pia
yatachochea uwekezaji katika sekta ya
mifugo.
“Hakuna mtu atakayewekeza katika kiwanda cha nyama kama hana
uhakika wa kupata ng’ombe wa kuchinja na
wenye ubora na kiwango kinachokubaliwa.
Jibu la kupata viwanda katika sekta hiyo kwa hiyo ni kuanzisha mashamba
ya kuzalisha malisho ya ng’ombe.
Nataka mpango wa kuanzisha
unenepeshaji wa ng’ombe nchi nzima
na kazi hiyo
ifanyike katika muda mfupi. Nataka
tuianze kazi hii haraka sana kwa sababu sekta ya
mifugo haiwezi kuendelea kubakia katika hali ya
ujima.”
Rais ametoa mfano wa nchi ya
Botswana ambayo imepata mafanikio makubwa katika mashamba ya kunenepesha ng’ombe.
“Botswana
ina ng’ombe kiasi cha milioni 1.8 na
uuzaji wa nyama nje ya
nchi unaiingizia nchi hiyo zaidi
ya dola za
Marekani milioni 20 kwa mwaka. Sisi
tunao ng’ombe kiasi cha milioni 20 na tunapata
nini katika fedha za kigeni?
Hata maofisa wa serikali
katika Botswana wameanzisha
mashamba ya kunenepesha ng’ombe.”
Kwa mujibu wa
wataalamu, ng’ombe anayenenepeshwa huongeza uzito wake kwa kilo mbili kila siku
na anakuwa tayari amepata uzito wa kutosha
wa kuingia sokoni kwa bei
nzuri katika muda wa miezi
mitatu. “Kazi hii ya kunenepa
haiwezi kufanywa na ng’ombe
aneyetembea kila saa na kila
siku. Hii shughuli ni ya ng’ombe
aliyekaa na kutulia.”
Katika mazungumzo yake, Rais Kikwete pia
ameelezwa baadhi ya kero zinazoikabili
sekta ya uvuvi na
ameahidi kusaidiana na viongozi wa
Wizara hiyo kumaliza kero hizo.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR
ES SALAAM.
30 Machi, 2011