DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

Rais Jakaya Kikwete amewataka viongozi mkoani Iringa kuwa mstari wa mbele kuwasaidia wananchi kubuni miradi yenye tija inayoweza kusaidia katika kuongeza kipato.

 

Rais Kikwete amewambia viongozi hao katika nyakati tofauti wakati wa kupokea taarifa za Wilaya Mkoani  hapa ambapo yuko katika ziara ya kikazi ya kukagua maendeleo na shughuli za wananchi kwa ujumla.

 

Viongozi ndiyo wakuelekeza wananchi kuibua miradi ya maendeleo na siyo kuwaachia wananchi, msiache majukumu yenu kwa wananchiAmesema.

 

Rais ametoa maelekezo hayo kwa viongozi baada ya kuwauliza viongozi juhudi wanazofanya za kutatua kero mbalimbali na kusaidia wananchi katika kuboresha maisha yao.

 

Katika sehemu kadhaa viongozi wamekuwa wakishindwa kubainisha kwa ufasaha na uwazi juhudi zao na majukumu ya kutatua kero  ambazo wananchi wamekuwa wanakumbana nazo na badala yake kumueleza Rais kuwa matatizo hayo hayajatatuliwa kwa sababu wananchi hawajaibua miradi.

 

Rais amewataka viongozi kuwa na mipango yao wenyewe ya maendeleo pale ambapo wananchi wameshindwa kuibua mipango na fursa mbalimbali za kimaendeleo kwani hilo ndiyo jukumu lao kubwa la msingi kama viongozi na siyo kuwaacha wananchi wakikabiliwa na matatizo kwa vile hawajaibua miradi.

 

Mkikamia kufanya maendeleo katika shughuli mbalimbali za kiuchumi mtawasaidia wananchi kupata maendeleo zaidi, ongezeni bidii ya ubunifu ili msaidie kuinua maisha ya wananchiAmeongeza, “Mnaweza kubadili wilaya na maeneo yenu kwa kusaidia wananchi kubuni na kuibua miradi na siyo kusubiri wao waibue ndiyo muanze kuifanyia kaziAmesema .

 

Rais ametoa mfano katika nyanja za kilimo ambapo wafugaji wanaweza kuongeza ubora wa mifugo yao kwa kutumia njia ya kuhimilisha (artificial Insemination), kuboresha ufugaji wa kuku wa kienyeji na hata kwenye shughuli mbalimbali za asili ambazo wananchi wanazimudu bila kuwa na utaalamu mkubwa.

 

Rais amesema ni jambo bora kama viongozi watakuwa mstari wa mbele kuhamasisha katika kuibua na kubuni njia mbalimbali za maendeleo tofauti na sasa ambapo viongozi wanasubiri wananchi waibue miradi au mipango yao wenyewe.

 

Rais amewakumbusha viongozi wa Iringa kuwa pamoja na ushirikishwaji wa wananchi katika shughuli zao za maendeleo , jukumu kubwa la viongozi ni kuwasaidia wananchi kwenda mbele zaidi na kamwe siyo kusubiri mpaka wao waje na mipango au miradi na kujiuliza kuwa itakuwaje pale ambapo wananchi hawajaibua au hawana uwezo wa kuibua miradi yeyote.

 

Rais amesema ameona wananchi wana jitihada kubwa mkoani Iringa za kujiletea maendeleo na kuridhishwa na juhudi hizo na hivyo viongozi hawana budi kushirikiana na kuongeza jitihada hizo katika mambo yanayoweza kuwaongezea kipato.

 

Wananchi katika Wilaya za Ludewa na Makete wametoa kilio chao cha kuchelewa kupata mbolea kwa wakati na umbali wa sehemu za kununulia mbolea hiyo.

 

Rais Amesema vitafunguliwa vituo vya kusambazia  mbolea katika wilaya za Ludewa na Makete ili kuwapunguzia wananchi adha hiyo.

 

Rais Kikwete anaendelea na ziara ya Kikazi  mkoani Iringa ambapo pia hutumia mikutano ya hadhara kupata maendeleo na matatizo ya wananchi kutoka kwa wenyeviti na viongozi na kisha kutoa majibu kupitia kwa wataalamu mbalimbali wakiwemo mawaziri aliofuatana nao, wataalamu wa Wizara mbalimbali na viongozi wa Mkoa.

 

Rais ameshatembelea Wilaya za Ludewa, Njombe, Makete na leo anatembelea Wilaya ya Mufindi.

 

Mwisho