DIRECTORATE
OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
UNITED
REPUBLIC OF TANZANIA
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116898
E-mail: press@ikulu.go.tz
Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S OFFICE,
THE
STATE HOUSE,
P.O. BOX 9120,
DAR
ES SALAAM.
Tanzania.
|
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais Jakaya Mrisho Kikwete
ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Korea
kwa kuchangia maendeleo ya Tanzania, mchango ambao ni pamoja
na kugharamia ujenzi wa daraja kwenye Mto Malagarasi, Mkoani Kigoma.
Aidha, Rais Kikwete ameishukuru
Jamhuri ya Korea
kwa kugharamia miradi ya sekta ya afya, na hasa
kukubali kuchangia katika ujenzi wa hospitali ya kisasa katika eneo la
Mulogazira, nje kidogo ya Dar es Salaam.
Rais Kikwete ametoa shukurani hizo, Ikulu,
Dar es Salaam, leo, Jumanne, Septemba 16, 2009, wakati alipozungumza na kuagana
na Balozi Young Jun Kim anayemaliza muda wake katika Tanzania baada ya kuwa
nchini kwa miaka mitatu.
“Nakushukuru sana kwa kuifanyia mengi
nchi yetu. Sasa Tanzania na Korea
zina uhusiano maridadi kabisa. Nakushukuru sana. Sasa tunayo
kila sababu ya kushangilia…Uhusiano wetu ni mzuri sana iwe kwenye ngazi ya
kisiasa ama kiuchumi,” amesema Rais Kikwete.
Kuhusu ujenzi wa
daraja kwenye Mto Malagarasi, Rais Kikwete amesema kuwa daraja hilo
litakuwa ni mnara wa kumbukumbu ya uhusiano kati ya Tanzania
na Jamhuri ya Korea.
Ujenzi huo umepangwa kuanza mwishoni
mwa mwaka huu kwa gharama ya sh bilioni 28.6 na
utarahisisha sana
mawasiliano kati ya Mkoa wa Kigoma na mikoa mingine.
Mbali na
kugharimia ujenzi wa daraja kwenye Mto Malagarasi, Jamhuri ya Korea imegharamia miradi mingine katika sekta za
maji katika wilaya za Chamwino na Bariadi katika mikoa ya Dodoma
na Shinyanga, na kwenye sekta ya afya ambako wanashiriki katika kuinua kiwango
cha vituo vitatu vya afya kuwa hospitali za wilaya katika Mkoa wa Dar es Salaam.
Rais Kikwete amemtaka balozi huyo
kuendelea kuwa rafiki mzuri wa Tanzania hasa kwa kuyashawishi makampuni zaidi
ya Korea kuja kuwekeza
katika uchumi wa Tanzania.
“Tunataka makampuni zaidi na zaidi ya Korea
kuja kuwekeza katika uchumi wa Tanzania.
Uchumi huu hautakua bila uwekezaji,” amesisitiza Rais.
Aidha, Rais ameishukuru Korea kwa mpango wake wa
kuleta wataalamu wa kujitolea kutoka Korea kuja kufanya kazi kwa muda
katika sekta mbalimbali nchini. “Nashukuru, sasa tuna
madaktari wengi zaidi, wahandisi wengi zaidi na walimu wengi zaidi kutoka Korea.”
Kiasi cha wataalam 100 wa namna hiyo sasa wanakuja Tanzania kwa
mwaka.
Rais pia amesema kuwa mpango wa Korea
wa kujenga vituo vya ufundi stadi nchini ni jambo muhimu katika kukuza na
kuboresha ujuzi wa Watanzania. Kwa sasa Korea iko katika mchakato wa kujenga vituo vya namna hiyo katika mikoa ya Lindi,
Pwani, Kigoma na Manyara.
Imetolewa
na:
Kurugenzi
ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR
ES SALAAM.
16
Septemba, 2009