UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumamosi, Machi 6, 2010, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Tanzania katika Japan, Mheshimiwa Salome Sijaona.

 

Katika mazungumzo hayo, Ikulu, Dar es Salaam, ambako Mheshimiwa Sijaona alikuwa anamuaga Rais Kikwete kabla ya kuondoka kwenda Japan kuanza majukumu yake mapya, Rais Kikwete amemshukuru mama huyo kwa kukubali uteuzi wake wa kuwa balozi katika nchi yenye uchumi wa pili kwa nguvu duniani.

 

Rais Kikwete amemwelezea Mheshimiwa Sijaona changamoto kuu tatu za Balozi wa Tanzania katika Japan, akianza kwa kumwambia kuwa moja ya shughuli zake kubwa lazima ziwe ni kufanya jitihada za kutangaza nafasi za uwekezaji katika uchumi wa Tanzania kutoka Japan.

 

Changamoto ya pili, amesema Mheshimiwa Rais, ni Balozi  huyo kujua kuwa Japan ni soko kubwa la bidhaa mbalimbali kutoka nje ikiwamo Tanzania na jinsi gani bidhaa za Tanzania zinavyoweza kuuzwa katika soko hilo.

 

 

Chukulia mfano wa kahawa ya Kilimanjaro, ambayo imekuwa maarufu katika Japan kwa sababu ya jitihada zilizofanywa na ubalozi wetu kuitangaza kahawa hiyo katika soko hilo. Tunaweza kabisa kuingiza bidhaa nyingine katika soko hilo kama tulivyofanya kwa kahawa,” amesema Rais Kikwete.

 

Mheshimiwa Rais amesema kuwa changamoto ya tatu kwa balozi huyo itakuwa ni kuongeza jitihada za kuvutia watalii zaidi kutoka Japan kuja kutembelea Tanzania. Wameanza kuja, lakini bado idadi ni ndogo, lazima kuongeza jitihada za kuwavutia Wajapan wengi zaidi kuja kutembelea vivutio vyetu vya utalii.”

 

Naye Balozi Mteule Sijaona amemwambia Rais Kikwete: “Nakushukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa imani yako kwangu, kwa kuniteua kushika nafasi hii. Nitafanya kila linalowezekana kufanikisha maelekezo yako na malengo ya nchi yetu.”

 

Mama Sijaona aliteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania katika Japan mwishoni mwa mwaka jana, wiki chache baada ya kuwa amestaafu kutoka utumishi wa umma wa miaka mingi, ambako pamoja na nafasi nyingine, alishikilia nafasi ya Ukatibu Mkuu wa wizara mbalimbali.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

06 Machi, 2010