UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Tanzania na Mozambique zitafungua ukurasa mpya wa mahusiano ya kidugu kati yao, Mei, mwaka huu, wakati viongozi wa nchi hizo mbili watakapozindua rasmi Daraja la Kihistoria la Umoja ambalo limekuwa ndoto ya miaka mingi  ya nchi hizo mbili.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemwambia Waziri Mkuu wa Mozambique, Mheshimiwa Aires Bonifacio Baptista Ali kuwa anakubaliana na pendekezo la Rais wa Mozambique, Mheshimiwa Armando Guebuza la kuzindua daraja hilo Mei 12, mwaka huu.

 

Rais Kikwete alikuwa anakutana na kuzungumza na Mheshimiwa Ali wakati Waziri Mkuu huyo mpya wa Mozambique alipokuja kumjulia hali Rais Kikwete leo, Jumamosi, Machi 6, 2010, Ikulu, mjini Dar es Salaam.

 

Mheshimiwa Ali yuko nchini kwa ziara ya kwanza nje ya Mozambique tokea alipoteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa Mozambique Januari 18, mwaka huu, wakati Rais Guebuza alipotangaza Baraza la Mawaziri jipya kufuatia ushindi mkubwa wa chama chake cha Frelimo katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana.

 

Kabla ya kuteuliwa kuwa Waziri Mkuu, kushika nafasi iliyokuwa inashikiliwa na Mheshimiwa Luisa Diogo, anayebakia bungeni lakini bila kuwa waziri, Mheshimiwa Ali alikuwa Waziri wa Elimu.

 

 

Daraja la Umoja lilianza kubuniwa na kuzungumzwa na nchi hizo mbili mwishoni mwa miaka ya 1970, kufuatia uhuru wa Mozambique mwaka 1975, lakini limeweza kujengwa na kukamilika katika Awamu ya Uongozi ya Rais Kikwete.

 

Daraja hilo liko katika eneo la Mtambaswala, Wilaya ya Nanyumbu, Mkoa wa Mtwara, na ujenzi wake ulikamilika  mwishoni mwa mwaka jana.

 

Wakati wa mazungumzo hayo, Rais Kikwete pia amesema kuwa amefurahishwa na makubaliano kati ya Tanzania na Mozambique ya kubadilisha wanafunzi wa vyuo vikuu.

 

Makubaliano hayo yamefikiwa mapema leo wakati Mheshimiwa Ali alipokutana na kufanya mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Pinda, kwenye siku ya kwanza ya ziara hiyo ya siku tatu.

 

Aidha, Rais Kikwete amempongeza Mheshimiwa Ali kwa kuteuliwa kwake kuwa Waziri Mkuu katika Serikali ya Mozambique, na kusema kuwa hana shaka kuwa uteuzi wake utazidi kuimarisha mahusiano ya kidugu na kidamu kati ya Tanzania na Mozambique.

 

Tumekuwa marafiki kwa miaka mingi, tumekuwa ndugu kwa muda mrefu na tutaendelea kuwa hivyo. Na zipo sababu za hali hiyo. Kwanza ni marafiki wa karibu ambako wananchi wetu wana ndugu kila upande wa  mpaka wa nchi zetu mbili”, amesema Mheshimiwa Rais Kikwete na kuongeza:

 

Pili, tulipigana pamoja katika Vita vya Ukombozi wa Mozambique, na baadaye kushirikiana kupambana na majangili na maharamia wenye silaha waliokuwa wanaisumbua Serikali ya Mozamboque. Vijana wetu wamezikwa pamoja na vijana wenu,”

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

06 Machi, 2010