UNITED REPUBLIC OF
TANZANIA
DIRECTORATE OF
PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116539 E-mail: press@ikulu.go.tz Website: www.mawasilianoikulu.go.tz Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S
OFFICE, THE STATE HOUSE, P.O. BOX
9120, DAR ES SALAAM. Tanzania. |
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete
leo, Alhamisi, Machi 31, 2011, amekutana na kufanya mazungumzo
na Waziri Mkuu wa Zimbabwe, Mheshimiwa Morgan Tsvangirai.
Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, mjini Dar es Salaam, Mheshimiwa Tsvangirai ambaye aliwasili nchini jana
usiku akifuatana na maofisa saba,
amemwelezea Rais Kikwete kuhusu hali ilivyo katika
Zimbabwe na ushirikiano ulivyo katika Serikali
ya Umoja wa Kitaifa nchini
Zimbabwe.
Rais Kikwete amemwambia Mheshimiwa Tsvangirai kuwa Tanzania itaendelea kuwa tayari kuisaidia
Zimbabwe kutatua matatizo yake hasa yale ya kisiasa
na pia kuisaidia
Serikali ya Umoja wa Kitaifa
ili iweze kutekeleza majukumu yake.
“Sisi katika Tanzania tunataka kuiona Zimbabwe yenye amani, Zimbabwe yenye mafanikio na tuko tayari kusaidia kwa namna yoyote
ambayo wananchi na Serikali ya
Zimbabwe inaona inafaa,” Rais Kikwete amemwambia
Mheshimiwa Tsvangirai katika mazungumzo hayo.
Mheshimiwa
Tsvangirai ambaye aliwasili nchini jana usiku
akitokea Malawi yuko kwenye ziara ya
nchi za Jumuia
ya Maendeleo ya Kusini mwa
Afrika (SADC) kwa nia ya kuwaelezea
viongozi wa nchi hizo hali
ilivyo katika Zimbabwe na changamoto zinazoikabili
Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Kabla ya kuja Tanzania, Mheshimiwa Tsvangirai alikuwa ametembelea Jamhuri ya Angola, Botswana, Jamhuri ya Kidemokrasia
ya Congo (DRC), Jamhuri ya Namibia, Mozambique, Afrika Kusini, Ufalme wa Swaziland na
Zambia.
Mara
baada ya mazungumzo na Rais
Kikwete, Mheshimiwa Tsvangirai na ujumbe
wake wameondoka mjini Dar es salaam kwenda Livingstone,
Zambia kuhudhuria mkutano wa nchi tatu
zinazounda Kamati Maalum (Troika) ya Siasa, Ulinzi na
Usalama ya SADC inayokutana leo.
Kamati hiyo iliyoundwa Juni mwaka 1996 ndiyo yenye jukumu
ya kujadili na kutafuta
njia za kumaliza
matatizo ya kisiasa katika eneo la nchi wanachama
wa SADC na nchi tatu zinazounda
Kamati hiyo kwa sasa ni
Zambia, Afrika Kusini na Mozambique.
Rais
Rupiah Bwezani Banda wa Zambia atakuwa mwenyekiti wa kikao
hicho ambacho pia kinahudhuriwa na Rais Jacob Zuma
wa Afrika Kusini na Rais
Armando Emilio Guebuza wa
Mozambique.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR
ES SALAAM.
31 Machi, 2011