UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amewashukuru Watanzania, na hasa Kamati ya Taifa ya Maandalizi, kwa kufanikisha mkutano mkubwa wa kimataifa wa uchumi wa World Economic Forum on Africa 2010 uliofanyika majuzi nchini.

 

Aidha, Rais Kikwete ametoa shukurani za pekee kwa wakazi wa Dar es Salaam waliojitokeza kwa wingi kuwalaki wageni wa mkutano huo na kuwa wavumilivu kwa kipindi chote cha mkutano pamoja na usumbufu wa hapa na pale.

 

Rais Kikwete pia ametoa changamoto ya Tanzania kutumia uzoefu uliopatikana katika maandalizi ya mafanikio makubwa ya mkutano huo, kuvutia mikutano mingine ya kimataifa iweze kufanyika nchini. Mkutano wa WEF on Africa 2010 uliofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Mlimani City Conference Centre Mei 5 hadi 7.

 

Rais Kikwete alikuwa akizungumza jana, Ijumaa, Mei 14, 2010, katika halfa ya chakula cha usiku kilichoandaliwa kwa ajili ya kuwapongeza watu waliokuwa mstari wa mbele katika kufanikisha mkutano huo wakiongozwa na Kamati ya Taifa ya Maandalizi ya mkutano huo chini ya uongozi wa Katibu Mkuu Kiongozi, Ndugu Philemon Luhanjo.

 

Rais Kikwete aliwaambia washiriki wa chakula hicho kwenye Hoteli ya Movenpick mjini Dar es Salaam:

 

“Ndugu zangu, nimeona ni vyema tukutane, tupate chakula cha usiku pamoja kwa ajili ya kuwapongeza kwa kazi mliyoifanya ya kuhakikisha kwamba Mkutano wa Kimataifa wa Uchumi Duniani Kuhusu Afrika unafanyika nchini kwetu kwa mafaniko makubwa.”

 

Akiwashukuru wakazi wa Dar es Salaam, Rais Kikwete alisema: “Shukurani za pekee ziwafikie wakazi wa Jiji la Dar es Salaam kwa kujitokeza kwa wingi kuwalaki wageni wetu, walikuwa wavumilivu kwa kipindi chote cha mkutano, najua kulikuwa na usumbufu wa hapa na pale hasa kwa upande wa barabara. Lakini mlivumilia kwa mapenzi ya nchi yenu na ukarimu wetu kwa wageni wetu. Nawashukuruni sana.”

 

Rais Kikwete pia ameyashukuru makundi maalum kwa mchango maalum katika kufanikisha mkutano huo ikiwa ni pamoja na madaktari na wauguzi, vyombo vya ulinzi na usalama na hasa askari wa usalama barabarani, na vikundi vya burudani vilivyotumbuiza katika halfa ambayo Rais aliwaandalia wageni wa mkutano huo.

 

Rais pia ametoa shukurani maalum kwa wafadhili wa mkutano huo yakiwamo makampuni ya Seregenti Breweries, Bakhresa Group, mabenki ya NMB, CRDB na NBC, Precision Air, Barrick Gold Mine na Benki Kuu ya Tanzania.

 

Rais pia ameshukuru uongozi wa Uwanja wa Ndege wa Julius K. Nyerere, mahoteli yaliyowapokea na kuwahudumia wageni, vyombo vya habari na makundi mengine yote yaliyotoa mchango maalum wakati wa mkutano huo.

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

15 Mei, 2009