UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo, Alhamisi, Aprili 8, 2010, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Naibu Kansela wa Ujerumani, Dk. Guido Westerwelle ambaye yuko katika ziara ya siku mbili nchini.

 

Mkutano huo, uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam pia umehudhuriwa na Waziri wa Ushirikiano wa Maendeleo wa nchi hiyo ya Ujerumani, Dk. Dirk Niebel, na pia na Waziri wa Mambo ya Nje Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Bernard Membe. Dk. Niebel anaandamana na Dk. Westerwelle katika ziara hiyo.

 

Katika mazungumzo hayo, Mheshimiwa Rais Kikwete na Waziri Westerwelle wamezungumzia masuala mbalimbali ya kimataifa, masuala yanayohusu Afrika na yale yanahusu ushirikiano kati ya Tanzania na Ujerumani.

 

Rais Kikwete ametumia nafasi hiyo kumwelezea Dk. Westerwelle, kwa undani, kuhusu hali ya kisiasa na usalama katika eneo la Nchi za Maziwa Makuu na eneo la nchi zinazounda Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC).

 

Rais Kikwete pia amemwelezea mgeni huyo kuhusu hali ya kisiasa katika Zanzibar na hatua zinazochukuliwa kuleta maridhiano Visiwani humo, na juu ya hali ya uchumi wa Tanzania ambao pamoja na zahma ya kiuchumi duniani bado umeweza kukua kwa asilimia 5.7 mwaka jana.

 

Viongozi hao wawili pia wamejadili kwa kina hali ya Somalia, na hasa hali ya uharamia ambayo imekuwa tishio katika Pwani ya Mashariki ya Afrika, ikiwa na chimbuko lake katika nchi hiyo ya Somalia,

 

Waziri Westerwelle amemwomba Mheshimiwa Rais Kikwete msaada wa Tanzania katika kupambana na hali hiyo ambayo viongozi hao wawili wamekubaliana kuwa ni tishio kwa ustawi wa uchumi na usalama wa dunia.

 

Rais Kikwete pia amemhakikishia Waziri huyo kuwa Tanzania inaendelea kuunga mkono jitihada za Ujerumani kusaka nafasi ya kuwa mwanachama wa kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

 

Rais Kikwete ameishukuru Ujerumani kwa misaada yake katika ujenzi wa Makao Makuu ya EAC, na kwa misaada yake kwa Tanzania hasa katika maeneo ya huduma za maji, sekta ya afya, mchango wa Ujerumani katika Bajeti ya Tanzania, na kwa misaada mingine ya maendeleo.

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

08 Aprili, 2010