UNITED
DIRECTORATE
OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116539 E-mail: press@ikulu.go.tz Website: www.mawasilianoikulu.go.tz Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S OFFICE, THE STATE HOUSE, P.O. BOX 9120,
DAR ES SALAAM. Tanzania. |
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete
ameondoka nchini asubuhi ya leo,
Jumatano, Mei 25, 2011, kwenda
Addis Ababa, Ethiopia kuhudhuria mkutano
maalum wa wakuu wa nchi
za Umoja wa Afrika (AU).
Mkutano huo wa siku mbili utajadili
hali ya amani
na usalama katika Bara la Afrika kufuatia matukio ya karibuni na
yanayoendelea katika nchi za Libya, Sudan, Somalia na Ivory Coast.
Mkutano huo ulioanza mchana
wa leo
na utaendelea kesho asubuhi umeitishwa
kufuatia pendekezo la Tume ya Amani
na Ulinzi (PSC) ya AU lililotolewa katika mkutano wa Tume hiyo
uliofanyika Aprili 24, mwaka huu. Hadi Mei 20, 2011, pendekezo hilo
lilikwishakuungwa mkono na zaidi ya
nchi 38 ambayo ni idadi zaidi
ya theluthi mbili ambayo inatakiwa
kwa AU kuweza kuitisha mkutano maalum wa wakuu
wa nchi wanachama
wa AU.
Moja ya mambo yatayojadiliwa kwa kina katika kikao hicho ni
hali ya Libya, nchi ambayo imeingia
katika machafuko na vita kubwa tokea
nchi wanachama wa Umoja wa
Kujihami wa Ulaya (NATO) zilipoanza kuishambulia nchi hiyo kwa ndege
za kivita, ili kuunga mkono
waasi wa utawala wa Muammar Gaddafi ambaye amekuwa anatawala nchi hiyo kwa miaka
41.
Hali ya usalama katika
Libya ilianza kubadilika tokea Februari 16, mwaka huu, wakati
waandamanaji kati ya 600 na
700 walipoingia mitaani katika mji wa
pili kwa ukubwa wa Benghazi kupinga uongozi wa miaka mingi
wa Gaddafi.
Machi 17, 2011, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa
(UNSC), kwa kuombwa na nchi za
Kiarabu, lilipitisha Azimio 1973 la kuzuia ndege yoyote kuruka
kwenye anga ya Libya na siku
mbili baadaye nchi baadhi ya
nchi wanachama wa NATO zilianza kuishambulia Libya kwa ndege za kivita.
Hali ya Sudan ambayo inajiandaa kwa
ajili ya kuzaliwa kwa taifa
jipya la Sudan Kusini iliingia katika dosari kubwa wiki iliyopita wakati majeshi ya Sudan yaliposhambulia na kuvamia jimbo la Abyei lililoko mpakani wa pande
hizo mbili. Majeshi ya Sudan yalivamia jimbo hilo baada
ya majeshi ya Sudan Kusini kudaiwa kushambulia msafara wa Umoja
wa Mataifa (UN).
Hali hiyo imezua wasiwasi
miongoni mwa mataifa mbalimbali duniani kuwa inaweza
kuwa kikwazo katika kuiwezesha Sudan Kusini kwa
taifa huru hapo Julai 9, mwaka
huu, 2011.
Somalia inaendelea
kukabiliwa na
ukosefu mkubwa wa amani na
usalama na miaka 20 sasa ikiwa
haina Serikali huku ikiwa chimbuko
kubwa la uharamia katika eneo la mashariki mwa Afrika.
Ivory Coast itajadiliwa kwa maana ya wakuu wa
nchi hizo kupewa ripoti ya
hali ilivyo katika nchi hiyo
kufuatia Rais Alasane Quattara kuapishwa kuwa kiongozi wa nchi
hiyo hivi majuzi.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR
ES SALAAM.
25
Mei, 2011