DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail:  ikulumawasiliano@yahoo.com

              press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

Na Mwandishi Maalum,

 

Rais Jakaya Mrisho Kikwete amelitaka Taifa la Israel na Wapalestina kutafuta njia za haraka kukomesha mara moja mashambulizi ambayo yamesababisha vifo vya mamia ya watu wa nchi hizo mbili, na hasa wa Palestina.

 

Rais amesema kuwa mauaji yanayosababishwa na mashambulizi hayo yanatisha na kuwa lazima pande hizo mbili zifanye kila linalowezekana kukomesha mashambulizi hayo.

 

Tafuteni njia zote zinazowezekana na za haraka kukomesha mara moja mashambulizi haya. Mauaji haya yanatisha,” ndiyo ulikuwa ujumbe thabiti na mfupi wa Rais Kikwete wakati alipokutana na mabalozi wa Israel na Palestina katika Tanzania katika mikutano miwili tofauti iliyofanyika asubuhi ya leo, Alhamisi, Januari 8, 2008, Ikulu, mjini Dar es Salaam.

 

Rais Kikwete amezungumza na pande zote mbili akitaka zimalize zahama hiyo ambayo mpaka sasa imekwishakusababisha vifo vya karibu watu 600, wengi wao wakiwa Wapalestina kutokana na mashambulizi kutoka kila upande kwenda mwingine.

 

Rais Kikwete amemwambia balozi mpya wa Palestina katika Tanzania, Balozi Dk. Nasri Khalil Abu Jaish kuwa ni muhimu kwa kikundi cha Hamas kusimamisha mashambuzi yake dhidi ya Israel.

 

Haya mashambulizi ya Hamas, yanatoa kisingizo kwa Israel kushambulia na kuua watu wengi katika Gaza na hivyo lazima yakomeshwe,” Rais Kikwete amemwambia Balozi huyo.

 

Rais ambaye alikuwa anapokea hati za utambulisho wa balozi huyo, amemweleza balozi kuwa amemwandikia Rais Mahmoud Abbas wa Palestina barua ya kumliwaza kuhusu mauaji hayo katika Gaza.

 

Israel imekuwa ikilishambulia eneo la Gaza la Palestina kulipiza kisasi kwa mashambulizi ya makombora ya kutengeneza kwa mkono kutoka eneo la Gaza.

 

Eneo la Gaza la Palestina liko chini ya udhibiti wa Hamas wakati eneo la West Bank pia ya Palestina liko chini ya chama cha PLO kinachoongozwa na Rais Abbas.

 

Rais pia amemwambia Balozi huyo kuwa msimamo wa miaka mingi wa Tanzania kuwepo kwa mataifa mawilimoja ya Israel na jingine la Palestina- katika eneo hilo la Mashariki ya kati unabakia pale pale.

 

Katika mazungumzo yake na Balozi wa Israel, Bwana Jacob Kdeidar, Rais Kikwete amesema kuwa wakati ni kweli kuwa Israel inayo haki ya kujilinda dhidi ya mashambulzi ya Hamas, lakini bado taifa hilo limetumia nguvu nyingi mno kupita kiasi katika kulipiza kisasi.

 

Maoni yetu ni kwamba lazima mtafute njia za haraka kukomesha jambo hilo vinginevyo msimamo wa dunia utawageuka. Kama ni kuonyesha hasira yenu, tayari mmefanya vya kutosha. Ni maoni yetu thabiti kuwa mtafute njia kukomesha mauaji haya,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:-

 

Tayari mashambulizi yenu yameua zaidi ya Wapalestina zaidi ya 500. Mtapoteza heshima sana, mtapoteza kungwa mkono na dunia. Ni dhahiri kuwa hamwezi kuyatetea wala kuhalalisha mashambulizi ya namna hii.”

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

08 Januari, 2009