DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

BAADHI ya makubaliano makuu yaliyofikiwa kwenye kikao cha leo, Jumanne, Februari 24, 2009, Ikulu, Dar es Salaam kati ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete na uongozi wa Wizara ya Maliasili na Utalii, na taasisi zake, ikiwa ni mfululizo wa mikutano ya tathmini ya utendaji wa Serikali:

 

(a)             Kwamba msimamo wa Serikali kupiga marufuku uuzaji wa magogo nje ya nchi ubakie pale pale kwa sababu una manufaa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuwashawishi wafanyabiashara wa bidhaa za mbao kuuza nje bidhaa ambazo tayari zimeongezwa thamani.

 

(b)             Kwamba hatua zaidi zichukuliwe kuimarisha usalama wa misitu nchini kwa kuajiri walinzi wa misitu zaidi, kuwabana na kuwadhibiti maofisa wa Serikali waliopewa jukumu la kusimamia usalama huo lakini siyo waaminifu, kusisitiza miiko ya utumishi wa umma katika usalama wa misitu, na kuendeleza elimu ya umma kuhusu usalama wa misitu.

 

(c)              Kwamba juhudi ziongezwe katika kampeni ya uhamasishaji wa kupanda miti nchini kwa sababu liko pengo kubwa kati ya miti inayopandwa na ile inayokatwa kila mwaka. Imeelezwa kuwa utafiti uliofanywa mwaka 1992 unaonyesha kuwa wakati zinapandwa hekta 25,000 za miti, kiasi cha hekta 92,000 zinakatwa kila mwaka.

 

(d)            Kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii ianze programu ya haraka ya kutenga maeneo maalum kwa ajili ya kupanda miti inayokua haraka kama njia ya kuongeza kasi ya kupanda miti, kujenga akiba ya misitu kwa ajili ya matumizi ya nishati hasa kwa wakazi wa mijini, na hivyo kulinda misitu ya asili na ya kisasa ili isindelee kukatwa.

 

(e)              Kwamba uongozi wa Wizara ya Maliasili na Utalii usimamie na udhibiti zaidi sekta ya misitu kwa lengo la kuiwezesha sekta hiyo kuongeza pato la taifa kutokana na mazao ya sekta hiyo.

 

(f)               Kwamba jitihada ziendelee katika kufanya tafiti kutafuta nishati mbadala badala ya matumizi ya kuni, na pia kutekeleza matokeo ya tafiti ambazo tayari zimefanyika na kuthibitisha kuwa matumizi yanaweza kupunguza matumizi ya kuni nchini.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

24 Februari, 2009