DIRECTORATE
OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
UNITED
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116898 E-mail: press@ikulu.go.tz Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S
OFFICE, THE STATE HOUSE, P.O. BOX 9120,
DAR ES SALAAM. Tanzania. |
TAARIFA KWA
VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amekitaka Chama cha Wanasheria
nchini kutafuta njia za haraka kupunguza gharama za huduma ya sheria nchini
ambazo amesema kuwa ni kubwa mno na zinawanyima wananchi wengi zaidi nafasi ya
kupata huduma hizo kwa gharama nafuu zaidi.
Aidha, Rais Kikwete amekipongeza
chama hicho cha Tanganyika Law Society (TLS)
kwa kazi nzuri na ya miaka mingi ya kuwatumikia wananchi wa Tanzania kwa
kuhakikisha kuwa wanapata huduma za kisheria.
Rais Kikwete alikuwa anafungua
mkutano wa siku mbili wa nusu mwaka wa Chama hicho cha Tanganyika Law Society kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Chuo Kikuu cha
Dodoma (UDOM) mjini Dodoma leo, Ijumaa, Agosti 13, mwaka huu, 2010.
Rais Kikwete amewaambia wanasheria
hao: “Kwa bahati mbaya, kupata haki ya kisheria katika Tanzania limebakia kuwa jambo
ghali sana. Matokeo yake ni kwamba Watanzania walio wengi wanashindwa kupata
haki yao hii ya msingi. Wanashindwa kumudu gharama za kupatiwa huduma ya
kisheria wakati wanapoihitaji.”
Rais amesema kuwa hali hiyo ni
lazima itafutiwe ufumbuzi wa haraka. “Hili ni jambo ambalo haliwezi kuachiwa
kuendelea. Lazima zichukuliwe hatua kufuta picha iliyojengeka kwamba taaluma
yenu ni ghali mno, haiendi kwa wakati na kwa kasi stahili na kuwa bado ina mapungufu
makubwa katika kujali wenzetu katika jamii yetu wenye uwezo mdogo zaidi.”
Ameongeza Rais Kikwete: “Wananchi
wengi wasiokuwa na uwezo miongoni mwetu wasiachiwe kupoteza matumaini yao ya
kupata haki zao za kisheria katika nchi ambako hakuna ukosefu wa wanasheria.”
Rais Kikwete pia amewataka wanachama
wa TLS kuchukua hatua za kukabiliana na masuala ya ukosefu wa maadili na
nidhamu miongoni mwa wanataaluma wa chama hicho.
“Naambiwa kuwa chama hiki kina mfumo
wa kushughulika na masuala ya nidhamu ya wanachama wake. Nasikitika kusema kuwa
ukosefu wa ufanisi wa mfumo huu umewaacha watu wengi wakitoa malalamiko yao
dhidi ya baadhi ya wanachama wenu wenye sifa mbaya bila kupata ufumbuzi wa
matatizo haya,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“Ukomavu wa kitaaluma wa chama chenu
unazo nguvu za kutosha kuwawezesha kupambana na wale ambao wanachafua jina na
heshima yenu nzuri ambayo ni matokeo ya kazi ya miaka mingi.”
Amesisitiza Rais Kikwete “Naambiwa
kuwa kilio cha gharama kubwa za huduma ya kisheria kingeweza kupungua kama nyie
wanachama wa TSL mngeendelea kuegemea na kufuata misingi yetu ya maadili na
sheria zenu wenyewe kuhusu malipo ya huduma za kisheria, ambayo naambiwa kuwa
inavunjwa zaidi kuliko kufuatwa.”
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES
SALAAM.
13 Agosti, 2010