UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116539

E-mail: press@ikulu.go.tz

Website:  www.mawasilianoikulu.go.tz  

Fax: 255-22-2113425

 

Coat of Arms

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

SALAMU ZA RAMBIRAMBI ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE

 

            Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Hajat Amina Mrisho kutokana na ajali mbili tofauti za barabarani zilizotokea mwishoni mwa wiki.

 

            Ajali ya kwanza iliyohusisha basi aina ya Toyota Coaster na lori lenye tela, ilipoteza maisha ya watu 14 na kujeruhi wengine 12.  Ajali hiyo ilitokea eneo la Mbala-Vigwaza katika Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani kufuatia basi hilo kuligonga kwa nyuma lori lenye tela.

 

            Ajali nyingine iliyotokea siku hiyo hiyo ilihusisha malori matatu ambayo yaligongana katika eneo la UbenaZomozi Wilayani Bagamoyo katika mkoa huo huo wa Pwani ambapo watu watatu walipoteza maisha na wengine sita kujeruhiwa.

 

            Kupotea kwa maisha ya watu hao 17 ni hasara kubwa kwa Taifa kutokana na umuhimu waliokuwa nao wakati wa uhai wao kwa maendeleo na ustawi wa nchi yetu”, amesema Rais Kikwete.

 

            Amesema kupoteza maisha kwa watu hao kumemhuzunisha zaidi kwa kuona kwamba ni siku chache tu zilizopita tangu Taifa lipoteze maisha ya wasanii 14 wa muziki wa Taarab katika ajali ya barabarani.

 

            Kupitia kwa Mkuu huyo wa Mkoa, Rais Kikwete ametuma salamu za rambirambi kwa familia za watu wote waliofariki katika ajali zote mbili huku akimwomba Mwenyezi Mungu azilaze mahali pema peponi roho za marehemu hao.

 

            Rais Kikwete amesema anawahakikishia wafiwa wote kuwa yuko pamoja nao katika msiba huo mkubwa, na amewaomba wawe wavumilivu na wenye subira katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo ya wapendwa wao.

            Aidha Rais Kikwete anawaombea kwa Mwenyezi Mungu majeruhi wote waweze kupona haraka na kurejea katika hali zao za kawaida na kuungana tena na ndugu, jamaa na marafiki zao na kuendelea na maisha kama mwanzoni.

 

            Rais Kikwete amezikumbusha mamlaka zote zinazohusika na usimamizi wa usalama barabarani kuongeza jitihada za kusimamia usalama wa watu wanaosafiri, ili Taifa lisiendelee kupoteza nguvu kazi yake kutokana na ajali za barabarani.

 

            Mwisho.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

29 Machi, 2011