DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

SALAMU ZA RAMBIRAMBI ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE

 

           

            Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mheshimiwa William Lukuvi kutokana na vifo vya watu 10 waliopoteza maisha kwa ajali ya barabarani baada ya lori kubwa la mafuta lenye tela kugongana na basi dogo la abiria aina ya Hiace na hatimaye kulilalia na kusababisha watu wote waliokuwemo kwenye basi hilo kufariki.  Ajali hiyo ilitokea eneo la Kibamba nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

 

          Kupitia kwa Mheshimiwa Lukuvi, Rais Kikwete ametuma salamu za rambirambi kwa wote walipoteza ndugu zao katika ajali hiyo mbaya. “Kupitia kwako, ninatuma salamu za rambirambi kwa watu wote waliopoteza ndugu, jamaa na marafiki katika ajali hiyo mbaya,” amesema Rais Kikwete katika salamu zake, na kuongeza, “ninaelewa fika ni kwa kiasi gani hivi sasa ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu wanaelemewa na huzuni kubwa na majonzi baada ya kuwapoteza wapendwa wao”.

 

          Amewaomba wafiwa wote wawe na moyo wa uvumilivu na ujasiri wakati huu mgumu wa maombolezo ya vifo vya ndugu, jamaa na marafiki zao na amemuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema azilaze roho za marehemu wote mahali pema peponi.

 

 

          Katika salamu zake hizo, Rais Kikwete amezisisitizia mamlaka zinazohusika na Sheria ya Usalama Barabarani kuisimamia kikamilifu sheria hiyo ili Taifa lisiendelee kupoteza watu wake kutokana na kukiukwa kwa sheria hiyo.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

26 Machi, 2010