DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

SALAMU ZA RAMBIRAMBI ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE

 

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi na pole nyingi Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mheshimiwa Injinia. Dkt. James Alex Msekela kutokana na vifo vya watu 22 watu 18 kati yao wakifa papo hapo tarehe 7 Agosti, 2010, baada ya basi dogo aina ya Toyota Hiace walilokuwa wakisafiria kutoka Kiteto kwenda Kondoa kugongana uso kwa uso na lori aina ya Scania kilometa chache kutoka Mondo wilayani Kondoa.

 

Nimeshtushwa, nimesikitishwa na kuhuzunishwa sana na taarifa za kupotea kwa maisha ya Watanzania wenzetu 22 ambapo 18 kati yao walikufa papo hapo kutokana na ajali hiyo mbaya na ya kutisha sana.  Inasikitisha na kuhuzunisha zaidi kwa vile familia ya watu watano akiwemo baba wa familia ilitekekea katika ajali hiyo,  amesema Rais Kikwete akiomboleza msiba huo kwenye salamu zake.

 

Ninaelewa huzuni kubwa waliyo nayo waliofikwa na msiba huo, hivyo kupitia kwako wewe Mkuu wa Mkoa, ninawatumia salamu za rambirambi na pole nyingi familia, ndugu, jamaa na marafiki waliopotelewa na wapendwa wao kwenye ajali hiyo.  Ninamuomba Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema azilaze mahali pema peponi roho za Marehemu wote, Amina”, ameongeza kusema Rais Kikwete.

 

Hata hivyo Rais Kikwete amesema, pamoja na majonzi makubwa waliyo nayo wafiwa, anawaomba wawe wavumilivu, watulivu na wenye moyo wa ujasiri katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo ya wapendwa wao, na kwamba yeye binafsi yuko pamoja nao katika msiba huo.

 

Kwa upande wa watu waliojeruhiwa katika ajali hiyo, Rais Kikwete anawaombea kwa Mwenyezi Mungu ili waweze kupona haraka na kuungana tena na ndugu na jamaa zao, hivyo kuendelea na maisha kama ilivyokuwa awali kabla ya kutokea kwa ajali.

 

Rais Kikwete amesema kwa vile ajali za barabarani zinaoneakana kukithiri katika siku za karibuni, amezitaka mamlaka zote zinazohusika na usimamizi wa Sheria ya Usalama Barabarani kubuni mbinu zitakazowezesha kudhibitiwa kikamilifu kwa ajali za barabarani ambazo zinasababisha kupotea kwa maisha ya watu wengi wasiokuwa na hatia, hivyo kulinyang’anya Taifa rasilimali muhimu isiyokuwa na mbadala kwa maendeleo ya nchi yetu.

 

Amesema hivi sasa angependa kuona hatua kali zikichukuliwa dhidi ya madereva wanaosababisha ajali hizo kwani nyingi zinaonekana kusababishwa na ukosefu wa umakini wa madereva wanaoendesha magari kwa mwendo wa kasi na hatimaye kushindwa kuyamudu inapotokea dharura yoyote barabarani.

 

Aidha, Rais Kikwete amesema ni wakati sasa wa kuangalia kama madereva wanapata mafunzo yanayostahili kwa kazi yao, na wasiokuwa na tabia za ulevi.  Vilevile amesisitiza kwamba vyombo vya usafiri hususan magari havina budi kukaguliwa mara kwa mara ili kujiridhisha na viwango vyao vya ubora.

 

“Nina hakika kwamba mambo yote hayo yakifanyika inavyopasa, Taifa letu litaondokana na jinamizi hili la ajali za barabarani na hivyo kuepuka vifo vya watu wengi vinavyotokea bila sababu za msingi”, amemalizia Rais Kikwete kwenye salamu zake za rambirambi.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

10 Agosti, 2010