DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

            Rais Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mheshimiwa Henry Shekifu kutokana na ajali mbaya ya barabarani iliyotokea jana tarehe 6 Agosti, 2009 katika kijiji na Kata ya Gehandu wilayani Hanang, Mkoani humo ambayo imesababisha vifo vya watu 10 na wengine 36 kujeruhiwa.

 

            Ajali hiyo ilitokea wakati basi la Kampuni ya Jordan lililokuwa likitokea  Arusha kwenda Mwanza  lilipopinduka mara kadhaa baada ya kuparamia ukingo wa daraja katika maeneo ya mpakani kwa Mikoa ya Manyara na Singida.

 

            “Ni kwa masikitiko na majonzi makuu ninakutumia wewe Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mheshimiwa Henry Shekifu salamu za rambirambi  kufuatia vifo vya watu 10 vilivyosababishwa na ajali mbaya ya barabarani iliyotokea jana tarehe 6 Agosti, 2009.  Kupitia kwako, natoa pia pole nyingi kwa watu wote waliojeruhiwa katika ajali hiyo huku nikiwaombea kwa Mwenyezi Mungu wapone haraka na wapate nafasi ya kuendelea na shughuli zao za kawaida”, amesema Rais Kikwete katika salamu zake.

 

            Katika salamu hizo, Rais Kikwete, hali kadhalika, amewatakia moyo wa uvumilivu na subira ndugu, jamaa na marafiki wa wote waliofariki katika ajali hiyo katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo ya wapendwa wao.

 

            Aidha katika salamu hizo za rambirambi, Rais Kikwete amerudia kukemea tabia ya ukiukwaji wa sheria ya usalama barabarani na hivyo kusababisha upotevu wa maisha ya watu  na uharibifu wa mali.

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

08 Agosti, 2009