UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail:  ikulumawasiliano@yahoo.com

              press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

SALAMU ZA RAMBIRAMBI ZA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHE. DK. JAKAYA MRISHO KIKWETE

 

            Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Said Kalembo kutokana na ajali mbaya ya barabarani iliyotokea tarehe 25 Julai, 2010 eneo la Segera, wilayani Korogwe katika mkoa wa Tanga na kusababisha watu 10 kupoteza maisha papo hapo na wengine wanane kujeruhiwa.

 

            Ajali hiyo ilihusisha magari mawili, moja likiwa basi dogo aina ya Toyota Hiace mali ya Kampuni ya Sayona Trans lililogongana uso kwa uso na lori la mafuta lenye tela aina ya Scania na hatimaye kuwaka moto uliochangia sana kuteketeza maisha ya abiria hao 10 waliokuwemo kwenye basi hilo na kuwajeruhi wengine.

 

            “Kwa dhati ya moyo wangu, nachukua fursa hii kukutumia salamu za rambirambi wewe Mkuu wa Mkoa kutokana na ajali hiyo iliyosababisha kupotea kwa roho za watu 10 wasiokuwa na hatia yoyote”, amesema Rais Kikwete katika salamu zake, na kuongeza, “kupitia kwako, natuma salamu za rambirambi na pole nyingi kwa familia zilizopotelewa na wapendwa wao kutokana na ajali hiyo, huku nikimuomba Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema aziweke mahali pema peponi roho zao, Amina”.

 

            Katika salamu hizo, pia Rais Kikwete amesema anawaomba wote waliofikwa na msiba huo mkubwa wawe na moyo wa uvumilivu na ujasiri wakati wote wa maombolezo.  Amesema anamuomba Mola awajalie wapone haraka wote waliojeruhiwa katika ajali hiyo na awawezeshe kuungana tena na ndugu, jamaa na marafiki zao ili waendelee na maisha kama kawaida.

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

27 Julai, 2010