DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail:  ikulumawasiliano@yahoo.com

              press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Suala la msingi katika mgogoro  wa Darfur nchini Sudan ni kuhakikisha usalama wa raia na mali zao kwanza ili kuweza kufanikisha juhudi zozote za kuleta amani na haki kwa wananchi wa jimbo hilo.

 

Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesema hayo leo  katika Ikulu ya Dar-Es-Salaam alipokutana na Dr. Mustapha Osman Ismail, Mwakilishi maalum wa Rais wa Sudan alipoleta ujumbe kutoka kwa Rais Omar Bashir.

 

“Usalama wa Raia ndiyo jambo la msingi ili kuwawezesha watu kupata  huduma na mahitaji yao muhimu ndipo tuweze kushughulika na mambo mengine”. Ameeleza na kufafanua kwamba suala la Haki na Sheria katika mgogoro huu ni muhimu pia lakini tunahitaji kuwa na kipaumbele katika kutatua mgogoro huu.

 

Rais pia ameongeza kuwa katika kufikia amani ya kweli ni jambo lililo wazi pia kwamba ushirikiano na ushirikishwaji wa serikali ya Sudan utahitajika kwa kiwango kikubwa.

 

Akielezea maendeleo ya juhudi mbalimbali zinazofanywa na jumuiya ya Kimataifa kutafuta amani ya kudumu katika jimbo la Darfur na Sudan kwa ujumla, Dr. Ismail amesema kikao cha usalama kinachotarajiwa kufanyika Abuja, Nigeria mwishoni mwa mwezi huu kitapokea na kupata taarifa mbalimbali za mapendekezo ya kutafuta amani na maridhiano katika jimbo hilo, ikiwa ni pamoja na ripoti ya mjumbe maalum wa Umoja wa Afrika, ambaye ni Rais wa Zamani wa Afrika ya Kusini Bw. Thabo Mbeki kuwasilisha ripoti ya kamati yake.

 

‘Tunaatarajia kuwa sasa tutajikita katika kutatua mgogoro huu wa Sudan kulingana na juhudi na mapendekezeo mbalimbali na tunategemea kuwa serikali ya Marekani nayo itaweka muongozo bora katika kutatua mgogoro huu ili kuweza kuendelea mbele.” Amesema Dr. Ismail.

 

Dr. Ismail ameishukuru Tanzania kwa kutoa mchango mkubwa katika suala la kutafuta amani katika jimbo la Darfur ambapo tayari timu ya wataalamu na maofisa kadhaa wameshakwenda Darfur na hivi karibuni inatarajia kuwa askari wapatao mia nane (800) watawasili katika jimbo hilo.

 

Dr. Ismail pia  ametumia nafasi hiyo  kumueleza Rais Kikwete kuwa Serikali ya Sudan imedhamiria kuimarisha urafiki baina wa  kibiashara, kijamii  na kisiasa baina ya nchi mbili hizi na pia kushirikiana katika masuala mbalimbali ikiwemo elimu.

 

Mwisho

 

Imetolewa na Premi Kibanga,

Mwandishi wa Habari wa Rais, Msaidizi

Ikulu-Dsm

20 Oktoba, 2009