UNITED
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116539 E-mail: press@ikulu.go.tz Website: www.mawasilianoikulu.go.tz Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S OFFICE, THE STATE HOUSE, P.O. BOX 9120, DAR ES SALAAM. Tanzania. |
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
RAIS
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amekialika
Kituo cha Ushirikiano wa Nchi Zinazoendelea cha South Centre cha Uswisi
kushiriki kikamilifu katika shughuli za kuazimisha miaka 50 ya uhuru
inayosheherekewa mwaka huu.
Rais
Kikwete ametoa mwaliko huo leo, Jumanne, Januari 25, 2011, wakati alipotembelea
Kituo hicho kilichoko mjini Geneva akakutana na kuzungumza na wajumbe wa Bodi na
wafanyakazi wa Kituo hicho kilichoko chini ya uenyekiti wa Rais Mstaafu
Benjamin William Mkapa. Kituo hicho kilianzishwa chini ya uongozi na uenyekiti
wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere katika miaka ya 1980.
Rais
Kikwete amewasili mjini Geneva asubuhi ya leo kwa ajili ya kuendesha kikao cha
kwanza cha Tume ya Kimataifa ya Kuzungumzia Afya ya Akinamama na Watoto
kinachofanyika kesho.
Rais
Kikwete ametoa mwaliko huo baada ya kusikiliza maoni ya baadhi ya wajumbe wa
Bodi ya Kituo hicho, akiwamo Chifu Emeka Anyaoku wa Nigeria na Rais Mkapa ambao
wote walisema kuwa njia bora zaidi ya kukumbuka uongozi wa mwalimu na mchango
wake kwa Tanzania, Afrika, na Jumuia ya kimataifa ni kwa South Centre kushiriki
kikamilifu katika sherehe za miaka 50 za taifa alilolianzisha.
“Nakubaliana
nanyi kuwa miaka 50 ya uhuru wetu ni miaka ya kusherehekea Kumbukumbu ya Maisha
ya Mwalimu Nyerere na yote ambayo ametufanyia sote – sisi Watanzania, sisi
Waafrika, sisi wana-jumuia ya kimataifa,” amesema Rais Kikwete katika mkutano
na Bodi hiyo na wafanyakazi wote wa South Centre.
Rais
Kikwete amekipongeza Kituo cha South Cenre kwa kazi nzuri inayofanywa na kituo
hicho katika kutetea maslahi ya nchi masikini zinazoendelea duniani kuhusu
masuala mbali mbali ya kimataifa na kusisisitiza kuwa kituo hicho kinafuata kikamilifu
nyayo za kweli kweli za Mwalimu Nyerere.
Rais
ameambiwa katika kituo hicho kuhusu masuala muhimu ambayo yamekuwa
yanashughulikiwa na Kituo hicho katika miaka mitatu iliyopita.
Masuala
hayo ni pamoja na Mikataba ya Ushirikiano wa Kiuchumi (EPA) isiyokubalika kati
ya nchi za Afrika na Carribbean, na zile za Umoja wa Ulaya (EU); zahama ya
kiuchumi duniani; suala la hatimiliki, hasa zile za dawa ambazo zinatishia
kupandisha sana bei ya dawa za binadamu duniani kwa namna ambayo hazitaweza
kununuliwa na watu masikini; pamoja na suala la mabadiliko ya tabianchi
lililoanza kuziathiri nchi masikini zaidi kuliko zile tajiri hata kama mchango
wa nchi masikini katika kuvuruga mazingira na mabadiliko ya tabia nchi ni
mdogo.
Akizungumza
kwenye mkutano huo uliofanyika kwenye makao makuu ya Kituo hicho cha South
Centre, Chifu Emeka Anyaoku amemwelezea Rais mstaafu Mkapa kama mwenyekiti
aliyefufua moyo wa Mwalimu katika maendeleo ya kituo hicho, na akamweleza Rais
Kikwete kama “mfuasi asiyepingwa wa Julius Mwalimu Nyerere”.
Rais
Mkapa ni mwenyekiti wa tano wa Bodi ya Kituo hicho ambacho mwenyekiti wake wa
kwanza alikuwa Mwalimu Nyerere. Wengine ambao wamekuwa wenyeviti wa Bodi ya
Kituo hicho ni Luis Fernando Jaramilla wa Colombia, Gamani Corea wa Sri Lanka
na Boutros Boutros Ghali wa Misri ambaye pia amepata kuwa Katibu Mkuu wa Umoja
wa Mataifa.
Mwisho.
Imetolewa na:
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais
Safarini,
Geneva.
25 Januari, 2011