DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail : press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

MHESHIMIWA RAIS AMEFURAHISHWA NA HATUA YA SERIKALI YA SUDAN YA KUANZISHA MCHAKATO WA KUMALIZA VITA.



Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa amefurahishwa na hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Sudan wa kuanzisha mchakato wa kumaliza vita ya Darfur.

 

Rais Kiwete pia ameitaka Serikali hiyo ya Rais Omar El Bashir kutafuta njia za haraka  kuanzisha majadiliano ya waasi nchini humo kama njia ya kuleta amani ya kudumu katika Sudan.

 

Rais Kikwete ameelezea matumaini yake hayo ya kukomeshwa kwa vita na zahama ya kibinadamu katika Darfur wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na mjumbe maalum wa Rais Bashir, Dk. Mustafa Osman, ambaye ni mshauri maalum wa kiongozi huyo wa Sudan.

 

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar Es Salaam, Dk. Osman ambaye amefuatana na Waziri wa Sheria wa Sudan, Sabidarat, mjumbe huyo maalum wa Rais Bashir amemwelezea Rais Kikwete hatua ambazo zimekuwa zinachukuliwa na uongozi wa nchi hiyo kumaliza vita ya Darfur ambayo imesababisha vifo vya maelfu ya watu.

 

“Nafurahi kusikia kuwa mmeanzisha mchakato wa ndani kujaribu kumaliza matatizo ya Darfur. Hatimaye, majibu ya mambo haya yote yako mikononi mwenu. Hii ni nchi yenu. Kazi yetu sisi ni kuwaungeni mkono,” amesema Rais Kikwete.

 

Viongozi hao wawili pia wamejadili kuhusu hati ya kukamatwa kwa Rais Bashir iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Uharifu (ICC) na athari zake katika kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa Darfur. ICC inataka Rais Bashir akamatwe na kushitakiwa kwa uharifu wa kivita.

 

Mjumbe huyo maalum wa Rais Bashir pia  amemwelezea Rais Kikwete kuhusu hali ya uhusiano ilivyo kati ya Sudan na Chad na juhudi ambazo zimekuwa zinafanyika kuondoa vikwazo vinavyosababisha mvutano kati ya nchi hizo mbili.

 

Mwisho.

 

Imetolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais

Ikulu.

Dar es Salaam.

14 Novemba, 2008