UNITED
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116539 E-mail: press@ikulu.go.tz Website: www.mawasilianoikulu.go.tz Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S OFFICE, THE STATE HOUSE, P.O. BOX 9120, DAR ES SALAAM. Tanzania. |
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, kesho,
Jumanne, Januari 25, 2011, ataongoza mkutano wa kwanza wa Tume ya Kimataifa Kuhusu
Afya ya Akinamama na Watoto utakaofanyika kwa siku moja mjini Geneva, Uswisi.
Rais
Kikwete amewasili mjini Geneva leo, Jumanne, Januari 25, 2011, tayari kuendesha
kikao hicho kwa ushirikiano na Waziri Mkuu wa Canada, Mheshimiwa Stephen
Harper, ambao ni wenyeviti wenza wa Tume hiyo iliyoundwa na Umoja wa Mataifa
(UN) kupitia Shirika la Afya Duniani (WHO).
Kazi
kubwa ya Tume hiyo yenye makamishna 30 na wazito kutoka maeneo mbali mbali ya
ujuzi na uzoefu duniani, itakuwa ni kuangalia njia za jinsi ya kupunguza vifo
vya akinamama na watoto na jinsi ya kuhakikisha kuwa Malengo ya Maendeleo ya
Milenia (MDG’s) katika maeneo ya afya ya akinamama na watoto yanaweza kufikiwa
ifikapo mwaka 2015, mwaka wa mwisho wa utekelezaji wa malengo hayo ya maendeleo
ya milenia.
Tume
hiyo pia itapendekeza njia bora zaidi ya kuziwezesha nchi mbali mbali duniani
kupata, kutunza na kutoa taarifa sahihi kuhusu afya ya akinamama na watoto na
jinsi nchi zinavyoweza kuwajibika zaidi katika matumizi ya fedha zinazotolewa
kimataifa kukabiliana na matatizo ya afya yanayowakabili akinamama na watoto.
Mkutano
wa leo utahudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mheshimiwa Ban Ki
Moon ambaye atashiriki katika ufunguzi, na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa
Mataifa, Mheshimiwa Dkt. Asha Rose Migiro ambaye vile vile ni kamishna wa tume
hiyo.
Wengine
ambao watahudhuria mkutano wa leo ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani
(WHO), Mheshimiwa Margaret Chan na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la
Mawasiliano ya Simu (ITU) Mheshimiwa Hamadoun Toure ambao wote wawili ni makamu
wenyeviti wenza wa mkutano huo.
Baada
ya kuwa ametoa hotuba kwenye shughuli ya ufunguzi wa mkutano huo, Rais Kikwete
atakuwa mwenyekiti wa kikao kitakachojadili uwajibikaji katika matumizi ya
fedha za kimataifa za kupambana na changamoto za kiafya zinazowakabili
akinamama na watoto na pia atakuwa mwenyekiti wa kikao cha majadiliano kuhusu
masuala mtambuka katika suala zima la afya za makundi hayo mawili.
Rais
Kikwete pia atazungumza kwenye kikao cha ufungaji wa mkutano huo na kwenye
mkutano wa kimataifa wa waandishi wa habari utakaofuatia shughuli ya ufungaji
wa kikao hicho.
Mwisho.
Imetolewa na:
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais,
Safarini,
GENEVA.
25 Januari, 2011