|
Ili kwenda sambamba na mabadiliko katika mfumo wa kiuchumi, Serikali ya
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania imechanganua upya wajibu wake kwa raia ambao ni pamoja na kutengeneza sera,
kulinda sheria za nchi, kutoa huduma muhimu za kijamii na miundo
mbinu ya kiuchumi na kusaidia maendeleo ya kiuchumi.
Serikali inatambua kwamba ina wajibu wa kusaidia sekta
binafsi na taasisi nyingine za kiuchumi katika juhudi zao za
kuwekeza katika shughuli za kuzalisha mali na biashara kwa
madhumuni ya kuharakisha ukuaji wa kiuchumi na maendeleo. Serikali
inaweza kufanya haya kwa kuweka sawa sera zinazofaa, kuweka
mazingira mazuri ya uwekezaji nchini na nje ya nchi, kusimamia
mabadiliko ya kitaasisi kwa minajili ya kusaidia maendeleo ya
sekta binafsi, kuchechemua imani ya wawekezaji kwa kuweka wazi
taratibu za kiutawala zilizo madhubuti katika Taasisi za serikali
na kuweka viunzi vya kanuni na sheria.
Kwa kutambua umuhimu huu wa kuandaa na kuweka mazingira mazuri kwa ajili
ya maendeleo ya sekta binafsi, serikali imekuwa ikifanya
mabadiliko katika taasisi na sera zake.
Serikali imelegeza masharti ya kiuchumi, imefanya
mabadiliko na kutunga sheria na sera mpya kadhaa zinazohusiana na
masuala ya uwekezaji. Aidha imefanya mabadiliko katika mfumo wa
fedha, imelegeza masharti ya biashara, na imeweka vivutio kwa
wawekezaji. Aidha imefanya juhudi mbalimbali kuinua na kuendeleza
sekta binafsi. Tanzania sasa imekuwa moja ya sehemu huru za
kuwekeza barani Afrika.
Katika kuunga mkono juhudi za sekta binafsi katika kusukuma maendeleo ya
jamii kiuchumi, serikali imeandaa utaratibu wa kurasimisha
uhusiano wake na sekta binafsi. Badala ya kukutana pale tu
inapotokea dharura sasa sekta binafsi inahusishwa katika kuandaa sera
zinazohusu sekta binafsi na nyinginezo (k.m. Sekta binafsi
imeshiriki katika Kamati ya Serikali ya Kuangalia Mfumo wa Kodi na
vikundi mbalimbali vya kuangalia Matumizi ya Serikali.) Aidha
Sekta binafsi pia imekuwa ikiwasiliana
na kutoa mchango wake mara kwa mara kwa serikali kupitia
taasisi nyingine kama Chama cha Wafanyibiashara wa Viwanda na
Kilimo Tanzania, Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania,
Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania na Baraza la Biashara la
Taifa ambalo limezinduliwa mwezi
April, 2001. Baraza la Biashara la Taifa jukumu lake kubwa ni
kutoa nafasi kwa sekta binafsi na za umma kushauriana juu ya
mikakati ya kukuza na kuendeleza uchumi.
Sekta binafsi imekuwa ikiyachukulia mabadiliko hayo kwa uangalifu mkubwa
na kuyaunga mkono. Ukiritimba katika Sekta ya fedha umeondolewa na
sasa kuna benki binafsi zaidi ya ishirini (20) na
Taasisi nyingine za fedha ambazo zinamiliki karibu asilimia
themanini (80%) ya
rasilimali katika mfumo wa benki. Soko la bima limefunguliwa kwa
makampuni binafsi ya hapa nchini na nchi za nje, na soko la kuuza
na kununua hisa limefunguliwa jijini Dar es Salaam. Zaidi ya
makampuni ya umma mia mbili na hamsini (250) kati ya mia nne (400)
yamebinafsishwa. Sekta ya Kilimo na miundo mbinu ambayo hapo awali
zilikuwa chini ya serikali zinazidi kubinafsishwa.
Viwanda mbalimbali vilivyokuwa chini ya umiliki wa serikali
vimebinafsishwa. Eneo ambalo limepata wawekezaji wengi zaidi
kutoka ndani na nje ya nchi ni utafutaji na uchimbaji madini
pamoja na utalii.
|