Ndugu
Wananchi,
Kwa
kutumia wataalam wazalendo, Serikali imeanzisha “Website” ya Taifa yenye
lengo la kudumisha na kuielezea taswira sahihi ya Tanzania kwa wananchi wake na
ulimwengu mzima. Itatoa pia taarifa sahihi kuhusu nchi yetu, kwa manufaa ya
wanaotaka kujua ukweli wa mambo. “Website” hii itatuwezesha na sisi
kushiriki kikamilifu katika utandawazi na hivyo kutangaza na kukuza utalii
pamoja na kuvutia wawekezaji. Aidha,
kupitia “Website” hiyo Serikali itaongeza uwazi katika shughuli zake na
kurahisisha upatikanaji wa habari za Tanzania katika mtandao wa kompyuta
unaotumika ulimwenguni, yaani “Internet”. Haya yote ni katika kudumisha
malengo ya uwazi na ukweli kama ambavyo nimekuwa nikizungumza katika hotuba
zangu nyingi.
“Website”
hii ya Taifa ina taarifa mbali mbali za Wizara za Serikali ya Jamhuri ya
Muungano, taarifa za kisekta, taarifa za kipekee kuhusu Zanzibar, na taarifa
nyinginezo nyingi kuhusu Tanzania. Hotuba
zangu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na hii ya kuadhimisha miaka arobaini ya uhuru
ambayo inasikika sasa hivi inaweza kupatikana katika “Internet” kupitia
Website ya Taifa. Aidha,
maadhimisho haya yanashuhudiwa moja kwa moja na watu mbalimbali ndani na nje ya
Tanzania kupitia “Internet”.
Ndugu
Wananchi,
“Website” hii ya
Taifa, ambayo anuani yake ni: www.tanzania.go.tz,
imekuwepo hewani kwa karibu mwaka mmoja hivi sasa kwa majaribio. Majaribio hayo
yamekuwa na mafanikio, na leo hii tunapoadhimisha miaka 40 ya Uhuru wetu,
ninaona fahari, na ninayo furaha kubwa, kutangaza kuwa ninaizindua
rasmi ‘‘Website’’ ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na ninatumia
fursa hii kuwataka viongozi wote na wananchi wanaoweza waende na wakati na
kutumia teknolojia za mawasiliano kama hizi za kisasa kwa ajili ya elimu,
burudani na biashara, lakini kwa mujibu wa sheria.
AHSANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA