Ulinzi na JKT

Muhtasari

Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iliundwa rasmi mwaka 1995. Kabla ya hapo, kati ya mwaka 1972 na mwaka 1989 majukumu ya Wizara hii yalikuwa yakifanywa na Wizara ya Nchi Ofisi ya Makamu wa pili wa Raisi. Kati ya mwaka 1989 na mwaka 1995 majukumu ya Wizara yalikuwa chini ya Waziri wa nchi ofisi ya Raisi. Aidha kabla ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar Wizara ilikuwa ikijulinana kama Wizara ya Ulinzi na Mambo ya nchi za nje.

Wizara ina jukumu kubwa la Kulinda Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (State Sovereignty) na Maslahi ya Taifa (National Interest) dhidi ya maadui wa ndani na nje.

Katika kutekeleza majukumu hayo Wizara ina taasisi zake kama ifuatavyo:-

i. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

ii. Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).

iii. Vyuo vya Mafunzo na Taasisi za Utafiti.

 

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa mfumo wa muundo wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ina wajibu wa kuhakikisha kuwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) linasaidia na kulinda nchi dhidi ya maadui wote wa ndani na nje na kusaidia mamlaka za kiraia. JWTZ lilianzishwa mwaka Septemba 01, 1964  baada ya maasi yaliyosababisha kuvunjwa kwa Jeshi la Kikoloni la  Tanganyika Rifles-TR.

Kufuatia Maasi hayo, Rais Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliamua kujumuisha JWTZ kwenye mfumo wa siasa na kwenye jamii inayoitumikia. Maofisa wa kijeshi na viongozi wa kisiasa walibadilishana nyadhifa jeshini, kwenye chama na Serikali. JWTZ lilikua jeshi pekee la Ulinzi na miongoni mwa majeshi ya taifa yaliyosaidia harakati za Ukombozi.  JWTZ imesaidia kutekeleza Sera ya mambo ya Nje na Ulinzi iliyoanzishwa mwaka 1964. Tanzaniailishiriki kwenye harakati za ukombozi kusini mwa Afrika kwa kutoa mafunzo kwa majeshi ya ukombozi katika kulinda nchi zao kutokana nakukandamizwa. JWTZ pia, limeshiriki kuzikomboa  nchi za Uganda na Msumbiji. Kusudio la kuanzishwa Jeshi la Mgambo lilikua ni kuwashirikisha wananchi katika Ulinzi wa nchi yao.

Jeshi la Kujenga Taifa -JKT lilianzishwa Julai 10,1964 kwa malengo ya kuwawezesha vijana wa Tanzania kujenga umoja wa kitaifa, Uzalendo na ukakamavu katika  kuhudumia nchi. JKT huwapa vijana mafunzo ya Kijeshi na stadi za kazi ili waweze kujitegemea. Jeshi la Kujenga Taifa na Jeshi la Akiba (Mgambo)  huliongezea nguvu za Kijeshi JWTZ pale inapohitajika

Uzalishaji Mali kupitia Viwanda

Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania - JWTZ limekuwa likijihusisha na shughuli mbalimbali za uzalishaji mali kupitia viwanda vyake kwa kutumia wataalamu wake wanajeshi na watumishi wa umma. Jeshi limekuwa likizalisha bidhaa mbalimbali zikiwemo zana za kilimo, mashine  na mitambo mbalimbali, malighafi zinazotumika katika ujenzi, kupitia viwanda na mashirika yake, kama Shirika la Uzalishaji mali la Jeshi la Kujenga Taifa- SUMA JKT lilianzishwa kwa lengo la kusaidia miradi ambayo ina uwezo mkubwa wa uzalishaji ili iweze kuzalisha zaidi na kwa faida na hivyo kuisaidia Serikali katika kupunguza matumizi ya kuendesha shughuli za JKT.

SUMAJKT ina viwanda vingi baadhi ya Viwanda hivyo ni kama Kiwanda cha Maji ya Uhuru Peak kijulikanacho SUMAJKT Bottling Plant kilichopo Mgulani, Kiwanda cha bidhaa za ngozi cha SUMAJKT Leather Products kilichopo Mlalakuwa Dar es Salaam, Kiwanda hiki huzalisha viatu vya aina mbalimbali na mikoba  na Kiwanda cha Ushonaji SUMAJKT Garments Co.Ltd  hii ni Kampuni ya Shirika la Uzalishaji Mali la JKT inayojishughulisha na ushonaji wa mavazi ya aina mbalimbali kwa ajili ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama, makampuni na watu binafsi kiwanda hiki kipo Mgulani JKT jijini Dar es Salaam.

 Shirika la Mzinga  Morogoro, Shirika hili hufanya tafiti mbalimbali za kijeshi, kuzalisha na kuuza zao la msingi, silaha za kiraia, baruti na viwashio kwa wachimbaji madini, mawe na wajenzi.   Shirika la NYUMBU lijulikanalo kama Tanzania Automotive Technology Centre- TATC lililopo  Kibaha Pwani,Shirika hili linajishughulisha  kuendeleza mapinduzi ya teknolojia za magari na mitambo nchini (Automotive Engineering). kwa kufanya utafiti na ubunifu ili Taifa liweze kujitegemea kiteknolojia

Nifanyeje kujiunga na JWTZ?

Uandikishaji

  • Mtu yeyote ataandikishwa kujiunga na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa sifa zifuatazo: -
  • Awe raia wa Tanzania
  • Awe na Elimu ya kidato cha nne na kuendelea na awe amefaulu..
  • Awe hajaoa/hajaolewa
  • Awe na umri kuanzia miaka 18 hadi 25
  • Awe na tabia na mwenendo mzuri
  • Awe na akili timamu na afya nzuri

Masharti ya Utumishi

  • Askari atapewa nambari ya utumishi baada ya kufaulu mafunzo ya awali.
  • Atalitumikia Jeshi kwa kipindi cha mwanzo cha miaka sita, baada ya hapo atafanya kazi kwa mkataba wa miaka miwili miwili kwa kibali cha Mkuu wa Majeshi.

Maafisa

Bodi ya Uteuzi wa Maafisa (Officers Selection Board) huwafanyia usaili Askari wenye elimu ya kidato cha sita na kuendelea toka Vikosini na Shule za Askari wapya (Recruitment Schools).

Watakaofaulu masailiano hayo hupewa hadhi ya Afisa Mwanafunzi (Officer Cadet), na hupelekwa Chuoni (Tanzania Military Academy) kwa mafunzo ya Uafisa kwa muda wa mwaka mmoja.  

Siku ya Mashujaa

Tanzania huadhimisha Siku ya Kuwakumbuka Mashujaa wetu waliopoteza maisha yao wakiutetea, kuupigania na kuulinda Uhuru wa Tanzania kila mwaka ifikapo Julai 25. Kama ilivyo desturi ya nchi yetu huadhimisha siku ya Mashujaa ambayo hutoa fursa ya kuwakumbuka mashujaa wa Tanzania waliojitolea maisha yao kwa ajili kupigania nchi yetu. Maadhimisho haya maalum hufanyika kitaifa katika mkoa ambao huteuliwa kwa ajili ya shughuli hiyo na hupambwa na gwaride rasmi la mazishi ambalo hufuatiwa na uwekaji wa silaha  mbalimbali za jadi kama ngao, upinde, mkuki, mashada ya maua na sime katika minara ya kumbukumbu za mashujaa iliyojengwa sehemu mbalimbali nchini

 

 

.

Sherehe za Uhuru

Kila mwaka ifikapo tarehe 09 Desemba Watanzania huadhimisha siku ya Uhuru wa Tanganyika, Sherehe hizi hufanyika Kitaifa katika Mkoa uliopendekezwa ambapo hupambwa na gwaride Maalumu la vyombo vya Ulinzi na Usalama wakiongozwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania -JWTZ.

Mgeni rasmi katika maadhimisho haya mara nyingi huwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Maadhimisho haya huwajumuisha wananchi na wageni mbalimbali kutoka nchi marafiki, mabalozi, viongozi wa Chama na Serikali.

Sherehe hizi ni sehemu ya kumbukizi kwa taifa kuonesha wapi tulipo, wapi tunakwenda  tangu tupate uhuru wetu tarehe 09 Desemba, 1961.

Siku ya Majeshi

Tarehe 01 Septemba ya kila mwaka ni ya Siku ya Majeshi,  Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania- JWTZ huadhimisha siku ya Majeshi ikiwa ni ishara ya kumbukizi ya  kuanzishwa kwa JWTZ. Siku  hii huwapa fursa ya kipekee Wanajeshi wote kufanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwa ni pamoja na kutoa huduma za afya bure kwa wananchi, kushiriki katika michezo mbalimbali, kufanya usafi katika maeneo ya wazi na yale ambayo hutumiwa na wananchi kama vile Masoko, vituo vya usafirishaji, maeneo ya hospitali, makambi na maeneo ya huduma za kitabibu. Hayo yote hufanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya kuanzishwa kwa JWTZ tangu tarehe 01 Septemba, 1964. Maadhimisho haya hufanyika kwa Jeshi zima nchini kote.

Siku ya Ulinzi wa Amani

nn

Mpangilio