Ofisi ya Rais - TAMISEMI

MUUNDO WA OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA

Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Ofisi ya Rais - TAMISEMI) inasimamia utekelezaji wa Sera mbalimbali za Kisekta na Sheria ya Tawala za Mikoa Sura 97, Sheria ya Serikali za Mitaa Mamlaka za Wilaya, Sura 287, Sheria ya Serikali za Mitaa Mamlaka za Miji Sura 288 na Sheria ya Tume ya Utumishi wa Walimu Sura 448. Ofisi ya Rais-TAMISEMI inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Hati ya Rais ya Mgawanyo wa Majukumu (Presidentrial Instrument) Namba. 144 ya tarehe 22 Aprili, 2016. Kimuundo Ofisi ya Rais-TAMISEMI ina Idara Tisa (9), Vitengo nane (8) na Taasisi Saba (7). Aidha, Ofisi ya Rais TAMISEMI inasimamia utekelezaji wa majukumu katika Mikoa 26, Wilaya 139, Halmashauri 184 ambazo kati yake Halmashauri za Majiji ni 6, Halmashauri za Manispaa 20, Halmashauri za Miji 21 na Halmashauri za Wilaya 137, Mamlaka za  Miji Midogo 71, Tarafa 570, Kata 3,956, Mitaa 4,263, Vijiji 12,318 na Vitongoji 64,384 hii ni mpaka 2020.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pia alitoa Notisi ya Mgawanyo wa Kazi za Wizara (Instrument) kupitia Gazeti la Serikali Na. 384 & 385 ya tarehe 7 Mei 2021 na marekebisho yake kupitia GN. Nambari 534 ya tarehe 2 Julai 2021. Katika Hati hiyo, Rais alianzisha Ofisi ya Rais - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ambayo ina jukumu la kutunga na kusimamia utekelezaji wa Sera za Ugatuaji wa Madaraka kwa Umma (D - by - D). Tawala za Mikoa na Tawala za Serikali za Mitaa na Maendeleo ya Miji na Vijiji. Wizara ina jukumu la kusimamia Tawala za Mikoa; Tawala za Serikali za Mitaa; Uratibu wa Huduma za jamii Vijijini na Mijini kama vile Usafiri, Afya, Maji na Usafi wa Mazingira; Tume ya Utumishi wa Walimu; Utambuzi na Maendeleo ya Wajasiriamali na Wafanyabiashara Wadogo; Utambuzi na Maendeleo ya Vipaji; Tawala za ElimuMsingi na Sekondari; Uboreshaji wa utendaji na maendeleo ya rasilimali watu; na Idara za Serikali, Mashirika ya Umma, Wakala, Programu na Miradi iliyo chini ya Ofisi hii. Aidha, majukumu ya Ofisi hii pia yanatokana na yafuatayo:-

 

  1. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara za 8 (1), 145 na 146 za mwaka 1977 na marekebisho yake yaliyofuata mara kwa mara. Ibara hizi zinaweka utaratibu wa Serikali za Mitaa, zikisisitiza kuwapa mamlaka wananchi na kusisitiza Serikali kuwajibika kwa wananchi. Pia inabainisha kuwa wananchi wana haki ya kushiriki, na kuanzisha hatua za uongozi katika kazi ya Mkoa, Wilaya na hata Kijiji;
  2. Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Na.7 ya 1982 (Sura ya 287), Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Na.8 ya 1982 (Sura ya 288). Katika Sheria hizi, Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa amepewa mamlaka ya kuanzisha Halmashauri za Wilaya na Miji;
  3. Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Na.9 ya mwaka 1982 (Sura ya 290) inampa mamlaka Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kukubaliana na Waziri wa Fedha kuhusu viwango vya ruzuku ya fedha kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa; na
  4. Sheria ya Tawala za Mikoa Na.19 ya 1997 (Sura ya 97). Sheria hii inaanzisha Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya, Afisa Tarafa, Sekretarieti ya Mkoa na Kamati za Ushauri za Mkoa (RCC) na Kamati za Ushauri za Wilaya (DCC).

KAZI NA MAJUKUMU YA OFISI YA RAIS-TAMISEMI

Majukumu na kazi za Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa zinatokana na majukumu yake. Zifuatazo ni kazi na majukumu ya Ofisi ya Rais TAMISEMI:-

 

  1.   Kuzijengea uwezo wa Tawala za Mikoa, Kuratibu na Kufuatilia masuala ya Mikoa na msaada wa kiufundi unaotolewa na Sekretarieti za Mikoa kwa Halmashauri;
  2.   Kuwezesha Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoa huduma bora;
  3.   Kuratibu usimamizi wa jumla na usimamizi wa elimu ya awali, msingi, sekondari, mahitaji maalum, elimu ya watu wazima na elimu isiyo rasmi;
  4.   Kuhakikisha maeneo ya vijijini na mijini yamepangwa ipasavyo yakiwa na maendeleo salama na endelevu katika nyanja za kiuchumi, kijamii, kimazingira na kisiasa;
  5.   Kuratibu, kusaidia na kuwezesha matengenezo na maendeleo ya miundombinu ya barabara ndani ya Halmashauri;
  6.   Kuratibu maingiliano muhimu ya OR-TAMISEMI na Wizara mama na Wizara za Sekta, Idara na Wakala, Watendaji wasio wa Serikali (Non State Actors), Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa;
  7.   Kuwezesha Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri kutoa taarifa na huduma bora na kwa wakati kupitia mifumo ya TEHAMA;
  8.   Kufanya ukaguzi wa kawaida, haki na ufanisi na ufuatiliaji wa fedha zinazotumwa kwenda kwenye Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa;
  9.   Kutoa utaalamu na huduma katika kuboresha Mifumo ya Usimamizi na Miundo ya Shirika kwa ufanisi na ili kutoa huduma bora kwenye Sekretarieti za Mikoa, Halmashauri na Taasisi zilizo chini ya OR-TAMISEMI;
  10.   Kutoa mfumo wa huduma za kisheria kwa Mikoa na Halmashauri kwa ajili ya kukuza na kuendeleza Serikali za Mitaa;
  11.   Kutoa usaidizi, mwongozo, uratibu, ufuatiliaji, juu ya kuwezesha usambazaji na utoaji wa usawa wa Huduma za Afya na Maendeleo ya Sekta ya Afya ndani ya Mikoa na Halmashauri;
  12.   Kutoa utaalamu na huduma katika usimamizi wa rasilimali watu na masuala ya utawala kwa OR-TAMISEMI;
  13.   Kutoa utaalamu na huduma katika uundaji wa sera, utekelezaji, ufuatiliaji na tathmini na mapitio yanayohusiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI;
  14.   Kutoa usimamizi mzuri wa mifumo ya udhibiti na usimamizi wa fedha kwa OR-TAMISEMI, Sekretarieti za Mikoa, Halmashauri na Taasisi zilizo chini ya OR-TAMISEMI;
  15.   Kutoa utaalamu na huduma katika masuala ya ununuzi, uhifadhi na usambazaji wa bidhaa na huduma;
  16.   Kutoa utaalamu na huduma katika masuala ya habari, mawasiliano na midahalo ya Umma na vyombo vya habari;
  17.  Kuwezesha Uchaguzi wa Serikali za Mitaa (Chaguzi za Ndogo) na;
  18. Kusimamia kazi za Taasisi zilizo chini yake.

VIPAUMBELE VYA OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA KWA MWAKA WA FEDHA 2023/2024

  1. Kusimamia shughuli za Utawala Bora, kukuza demokrasia, ushirikishwaji wa wananchi na Ugatuaji wa Madaraka kwa Umma (D by D);
  2. Kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli za utoaji wa ElimuMsingi na  Sekondari katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ikijumuisha utekelezaji wa ElimuMsingi na Sekondari Bila Ada;
  3. Kuratibu na kusimamia Mkakati wa kuongeza ukusanyaji wa mapato na kudhibiti matumizi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa;
  4. Kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli za utoaji wa Huduma za Afya ya Msingi, Ustawi wa Jamii na Lishe katika Mamlaka za Serikali za Mitaa;
  5. Kushughulikia malalamiko ya walimu ikiwemo kutopandishwa vyeo kwa wakati; na wastaafu  kucheleweshewa   kulipwa   stahiki na mafao yao baada ya kustaafu na kero zinazowakabili walimu waliostaafu;
  6. Kuchochea na kuhimiza ukuaji wa uchumi shindani kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla kwa kuiwezesha Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuweka mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji, hasa katika Kilimo, Mifugo na Viwanda. Utekelezaji wa jambo hili umehusisha uimarishaji wa Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji na Viwanda, Biashara na  Uwekezaji  katika ngazi ya Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuhakikisha kuna rasilimali watu wenye weledi pamoja na uwepo wa fedha na vitendea kazi;
  7. Kufanya Ukaguzi, Ufuatiliaji na Tathmini kuhusu utekelezaji wa shughuli za Taasisi, Programu na miradi katika ngazi ya Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa;
  8. Kusimamia mifumo na miundombinu ya TEHAMA katika ngazi zote za Ofisi ya Rais - TAMISEMI;
  9. Kujenga uwezo wa watumishi wa Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi;
  10. Kuratibu shughuli na utendaji kazi kwa Taasisi zilizopo chini ya Ofisi ya Rais - TAMISEMI;
  11. Kuratibu shughuli za  ujenzi,  matengenezo na ukarabati wa miundombinu ya barabara, usafirishaji, maeneo ya utawala na maeneo ya kutolea huduma za jamii kwenye Taasisi, Mikoa, Wilaya na Halmashauri;
  12. Kusimamia matumizi ya rasilimali fedha katika ngazi zote za Ofisi ya Rais  - TAMISEMI;
  13. Kuratibu uendelezaji wa Vijiji na Miji, na
  14. Kuratibu na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi kwa watumishi wa Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa.

 

Kishindo cha OR- TAMISEMI

  • Hadi Februari, 2022 vyumba vya madarasa 11,988 kati ya vyumba 12,000 vya Shule za Sekondari vimejengwa na kukamilika sawa na asilimia 99.99. Vilevile, vyumba vya madarasa 2,978 kati ya 3,000 vimejengwa na kukamilika katika Vituo shikizi sawa na asilimia 99.26.

 

  • Ofisi za walimu 3,184, matundu ya vyoo 557 yamejengwa, ajira zilizozalishwa 21,872 wakiwemo wanaume 17,354 na wanawake, 4,518, madawati 47,149 na seti ya meza na viti 451,918 vimetengenezwa.

 

  • Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeomba kibali cha kuajiri walimu 10,000 wa Shule za Msingi na Sekondari. Kati ya hao, walimu 5,000 ni kwa ajili ya shule za Awali na Msingi na 5,000 kwa ajili ya Shule za Sekondari. Hii itapunguza mahitaji ya walimu wa Shule za Sekondari kwa asilimia 6.56 na elimu ya Awali na Msingi kwa asilimia 10.65. 

 

  • Wanafunzi 907,803 waliofaulu mtihani wa darasa Saba mwaka 2021 kupata nafasi ya kuanza Kidato cha Kwanza Januari, 2022 bila kuwa na chaguo la pili.

 

  • Kupitia Programu ya Uboreshaji wa Elimu katika Shule za Sekondari (Secondary Education Quality Improvement Program-SEQUIP) jumla ya Shilingi bilioni 30 zimepokelewa ambapo kila Shule imepokea Shilingi bilioni 3.00 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Shule za Sekondari za masomo ya sayansi kwa Wasichana

Kwanini Anwani za Makazi?

Majukumu ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ni pamoja na kupanga, kupima, kugawa, kumilikisha na kusimamia uendelezaji wa makazi katika maeneo ya utawala. Utaratibu huu unahitaji ufanisi katika usimamizi na udhibiti wa uendelezaji wa makazi na matumizi mengine. Utaratibu uliopo ni wa kutoa vibali vya kuendeleza maeneo yote yaliyopimwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa baada ya kuzingatia masuala muhimu ya uendelezaji kama vile umiliki, matumizi ya Ardhi, upimaji na masharti mengine ya uendelezaji.

Hata hivyo, kutokana na kasi kubwa ya ongezeko la watu na mahitaji makubwa ya makazi, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeshindwa kukidhi matakwa ya kupima maeneo ya kutosha ambayo wananchi wanaweza kuendeleza makazi yao kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo. Hali hii imefanya majengo mengi kujengwa bila vibali vya ujenzi na mengine kuendelezwa kwenye maeneo yasiyopimwa hivyo kuleta changamoto ya uundaji wa anwani za makazi. Itazingatiwa kuwa utaratibu wa anwani za makazi ulikuwepo siku za nyuma hususani miongo miwili baada ya uhuru na kufifia baadae kutokana na mabadiliko mbalimbali ya kiutawala na kisiasa.

Kutokuwepo kwa majina ya barabara, njia na nambari za nyumba ikichangiwa na ukuaji wa maeneo ya mijini, inaleta tatizo kwa sababu huduma nyingi za miji zinaathiriwa zikiwa ni pamoja na huduma za kijamii, kiuchumi na miundombinu. Ili kuondokana na matatizo yaliyoelezwa hapo juu, Wizara zenye dhamana na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa pande zote za Muungano, zilipewa jukumu la kutoa Mwongozo kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini ili ziweze kutoa anwani za makazi kwa wananchi wote.Mwongozo wa Anwani za Makazi 

Mwongozo wa Utoaji wa Vibali vya Ujenzi na Usimamizi wa Ukaguzi wa Ujenzi wa Majengo

Ongezeko la kasi ya ujenzi ni moja ya sababu za Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwa na uwezo mdogo wa kupanga, kusimamia na kudhibiti uendelezaji na hivyo kufanya usimamizi wa ukaguzi wa ujenzi wa majengo uwe dhaifu na majengo kuwa na viwango hafifu na kukosa usalama. Ukaguzi wa ujenzi wa majengo haufanyiki inavyotakiwa hivyo, kuathiri ubora wa majengo.

Waendelezaji wengi hawatumii ipasavyo ushauri wa kitaalamu na baadhi ya Makampuni yasiyozingatia maadili ya kitaaluma huonyesha majina na ushiriki wao kwenye mabango yenye taarifa za Ujenzi. Wapo pia, wataalam wanao saini kwenye vitabu vya ukaguzi (Inspection books) bila ya kukagua jengo husika kama inavyotakiwa.

Mwendelezaji anao mchango mkubwa katika kufikia ubora wa jengo uliokusudiwa. Vile vile, ni wajibu wake kuzingatia maelekezo yote yaliyomo kwenye Kibali cha Ujenzi kilichotolewa. Iwapo atamwaajiri mtaalamu mshauri na mkandarasi mahiri na mwaminifu,itarahisisha kazi ya ukaguzi. Kumekuwepo na udhaifu kwenye usimamizi unaosababishwa na waendelezaji kuajiri wataalamu washauri wasio na sifa na baadhi yao kutotembelea maeneo ya Ujenzi kufanya ukaguzi.

Hivyo, Ofisi ya Rais –TAMISEMI iliandaa Mwongozo utakaotumika wakati wa kutoa Vibali vya Ujenzi na Usimamizi wa Ukaguzi wa Ujenzi wa Majengo kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. Mwongozo huu umeandaliwa ili kuondoa changamoto zilizopo kwenye utaratibu wa utoaji wa Vibali vya Ujenzi na usimamizi wa Ujenzi wa majengo.

Kwa mujibu wa Vifungu 124 na 125 vya Kanuni za Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) (Udhibiti Uendelezaji), Sura 288 (GN 242 ya mwaka 2008), Ujenzi wowote ndani ya Mamlaka za Upangaji ambazo ni Mamlaka za Miji Midogo, Halmashauri za Miji, Manispaa na Ma-jiji ni lazima upate kibali cha Ujenzi kutoka kwenye Mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Kifungu cha 35 (i) cha Sheria ya Mipangomiji Na. 8 ya mwaka 2007, Mamlaka ya Upangaji inatakiwa kutoa kibali cha Ujenzi katika kipindi kisichozidi siku 60 kuanzia tarehe mwombaji alipowasilisha maombi yake. Aidha, ndani ya muda huo mamlaka inatakiwa kumjulisha mwombaji kuwa amekubaliwa au amekataliwa ombi lake na kutaja sababu zilizopelekea ombi lake kukataliwa.

Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Kifungu 122(4) imezipa majukumu Mamlaka za Wilaya ya kutoa au kubadilisha majina, namba za barabara, mitaa na nyumba kama ilivyobainishwa kwenye Mwongozo wa Anwani za Makazi na Postikodi wa Agosti 2016. Kufanya hivyo, kutadhibiti uendelezaji holela wa Vijiji na Miji Midogo inayochipukia.

Mwongozo huu ukifuatwa kikamilifu, kwa kigezo cha kiashiria cha utoaji wa Vibali vya Ujenzi, utaboresha mazingira ya kufanya biashara na uwekezaji kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. Mamlaka hizo zinatakiwa kutoa Vibali vya Ujenzi ndani ya kipindi cha kati ya siku saba na mwezi mmoja. Pia, mwongozo utaboresha usimamizi wa ukaguzi wa Ujenzi wa majengo.Mwongozo wa Utoaji Vibali vya Ujenzi

Orodha ya Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI)

NA.

     TAASISI

 AINA YA TAASISI

 1. 

 Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC)

Idara Inayojitegemea

 2.

Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA)

Wakala wa Utendaji

 

 3.

Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART)

Wakala wa Utendaji

 4.

Shirika la Elimu Kibaha (KEC)

Taasisi ya Umma

 5.

Chuo cha Serikali za Mitaa (LGTI)

Taasisi ya Umma

 6.

Shirika la Masoko Kariakoo (KMC)

Shirika la Umma

 7.

Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa (LGLB)

Taasisi ya Umma

Mpangilio