Muungano

Historia ya Muungano

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliundwa tarehe 26 Aprili, 1964. Baada ya Muungano, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Sheikh Abeid Aman Karume akawa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Rashidi Mfaume Kawawa alikuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Tanzania na Kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni.

Mwaka 1992, Tanzania ilipitisha Mfumo wa Demokrasia ya Vyama Vingi ambao ulihitaji marekebisho makubwa ya Katiba. Marekebisho haya yalihusu suala la Makamu wa Rais na kuanzishwa mfumo wa mgombea mwenza uliowashirikisha mgombea Urais na Makamu wa Rais. Hii ilimaanisha kwamba, Rais wa Zanzibar aliacha kuwa Makamu wa Rais wa Muungano moja kwa moja lakini akawa Mjumbe wa Baraza la Mawaziri la Muungano.

Bonyeza chini kusoma Kitabu cha Historia ya Muungano

https://www.vpo.go.tz/uploads/publications/en-1677316979-Kitabu%20cha%20Historia%20ya%20Muungano%20wa%20Tanganyika%20na%20Zanzibar.pdf

Sababu za kufanyika Muungano

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umekuwepo kutokana na sababu mbalimbali kama vile kuwepo kwa mahusiano ya karibu na ya kihistoria baina ya Tanganyika na Zanzibar katika nyanja mbalimbali kama vile udugu wa damu, biashara, utamaduni, lugha na mahusiano ya karibu kisiasa hususan baina ya vyama vya TANU na ASP.

Pia, adhma ya kuwa na Muungano wa Afrika hususan kwa kuanzia na Shirikisho la Afrika Mashariki. Hata kabla ya uhuru wa Tanganyika, Mwalimu Nyerere pamoja na viongozi wengine waliokuwa wakipigania uhuru katika ukanda wa Afrika walikuwa na matarajio ya kuwa na Muungano wa Afrika. Mwalimu Nyerere binafsi alipendelea uwepo Muungano wa Afrika kwa kuanzia na Mashirikisho ya kikanda.

Kimsingi zipo sababu mbalimbali zilizosababisha Muungano huu kama vile historia za nchi hizi mbili, ukaribu wa nchi hizi mbili, muingiliano wa kijamii, ushirikiano wa kibiashara, ushirikiano madhubuti na wa muda mrefu wa kisiasa baina ya TANU na ASP, ushirikiano na urafiki wa muda mrefu kati ya watu, viongozi, na wakati wa harakati za utaifa uliopelekea uhuru wa nchi hizo mbili. 

Hati ya Makubaliano ya Muungano

Msingi wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ni Hati za Muungano za mwaka 1964. Hati za Muungano zilitiwa saini na waasisi wa Muungano tarehe 22 Aprili, 1964, na kupelekea Tanganyika na Zanzibar kuwa dola moja ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Baada ya Muungano, Mwalimu J. K. Nyerere alikuwa Rais wa kwanza wa Jamhuri ya ya Muungano wa Tanzania na Sheikh Abeid Amani Karume, alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aprili 26, 1964 Bunge la Tanganyika lilipitisha Sheria za Muungano.Halikadhalika, Sheria hizi zilithibitishwa na Baraza la Mapinduzi Zanzibar. Sheria hizi za Muungano zilithibitisha Hati za Muungano, zilitaja Rais na Makamu wa Rais, zilitaja Muundo wa Muungano na Katiba ya Muungano.

Aidha, Aprili 27, 1964, waasisi wa Muungano walibadilishana Hati za Muungano na wajumbe saba wa Baraza la Mapinduzi waliapishwa kuwa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao ni Sheikh Abeid Amani Karume, Kassim Abdala Hanga, Abdulrahaman Mohamed Babu, Hassan Nassor Moyo, Sheikh Aboud Jumbe, Hasnu Makame na Sheikh Idris Abdul Wakil. Baada ya kuapishwa kuwa Wabunge wakateuliwa kuwa Mawaziri wa Serikali ya Muungano.

Hoja za Muungano zilizopatiwa ufumbuzi na zinazoendelea kutafutiwa ufumbuzi

Hoja zilizopatiwa ufumbuzi katika kikao hicho ni kama ifuatavyo;

  1. Malalamiko ya Wafanyabiashara wa Tanzania Zanzibar kutozwa kodi mara mbili wanapoagiza mizigo kutoka nje ya nchi na kupeleka Tanzania Bara
  2. Kodi ya Mapato na Kodi ya Zuio.
  3. Ongezeko la Gharama za Umeme kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwenda Shirika la Umeme (ZECO)
  4. Hoja ya Mkataba wa Mkopo wa Fedha za Mradi wa Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume (Terminal III).

Hoja nne za Muungano zinazoendelea kutafutiwa ufumbuzi

  1. Mgawanyo wa Mapato yatokanayo na Hisa za SMZ zilizokuwa katika Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki na faida ya Benki Kuu
  2. Mapendekezo ya Tume ya 13 Pamoja ya Fedha
  3. Usajili wa Vyombo vya moto
  4. Uingizaji wa sukari inayozalishwa Zanzibar katika soko la Tanzania Bara.

Yajue Mambo 22 ya Muungano

 

  1. Katiba ya Tanzania na Serikari ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
  2. Mambo ya Nchi za Nje
  3. Ulinzi na Usalama
  4. Polisi
  5. Mamlaka juu ya mambo yanayohusika na hali ya hatari
  6. Uraia
  7. Uhamiaji
  8. Mikopo na Biashara ya Nchi na Nje
  9. Utumishi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano
  10. Kodi ya Mapato inayolipwa na watu binafsi na mashirika, ushuru wa forodha na ushuru wa bidhaa zinazotengenezwa nchini Tanzania unaosimamiwa na Idara ya Forodha
  11. Bandari, Mambo yanayohusika na Usafiri wa Anga, Posta na Simu
  12. Mambo yote yanayohusika na sarafu na fedha kwa ajili ya malipo yote halali (pamoja na noti); mabenki (pamoja na mabenki ya kuweka akiba) na shughuli zote za mabenki; fedha za kigeni na usimamizi juu ya mambo yanayohusika na fedha za kigeni
  13. Leseni za Viwanda na Takwimu
  14. Elimu ya Juu
  15. Maliasili ya mafuta, pamoja na mafuta yasiyochujwa ya Motokaa na Mafuta ya aina ya Petroli na aina nyinginezo za mafuta au bidhaa, na Gesi asilia
  16. Baraza la Taifa la Mitihani la Tanzania na mambo yote yanayohusika na kazi za Baraza hilo
  17. Usafiri na usafirishaji wa anga
  18. Utafiti
  19. Utabiri wa Hali ya Hewa
  20. Takwimu
  21. Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano
  22. Uandikishaji wa vyama vya siasa na mambo mengine yanayohusiana na navyo
Mpangilio